Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA UHAI WANGU 9

MUENDELEZO Baada ya huduma zote hizo Mike alimlipa dereva kiasi cha shilingi elfu tisa kwa kazi yake aliyoifanya. "Pole sana bw...

Image result for siku za mwisho za uhai wangu 7

MUENDELEZO


Baada ya huduma zote hizo Mike alimlipa dereva kiasi cha shilingi elfu tisa kwa kazi yake aliyoifanya.
"Pole sana bwana, tuombe Mungu amnusuru mgonjwa wetu!"
"Asante sana umenisaidia sana, bila wewe sijui kama ningeweza!"
"Usijali!"
Kabla dereva hajaondoka Mike alikumbuka kitu.
"Nimeacha gari langu mtaa wa Nyerere, karibu kabisa na mnara wa saa, hebu naomba uchukue hizi funguo ukaliondoe hapo lilipo ulipeleke nyumbani kwangu!"
"Ni gari la aina gani bwana?" Aliuliza yule dereva wa teksi.
"BMW!" Alijibu.
"Unaishi wapi rafiki?"
Mike alimwelekeza yule dereva nyumbani kwake na baada ya kuelewa dereva aliondoka kuelekea mjini.
Mike alibaki amekaa kwenye benchi nje ya chumba cha wagonjwa mahututi hakutaka kuondoka, alitaka auone mwisho wa maisha ya mpenzi wake. Akiwa katikati ya mawazo, ghafla mlango ulifunguliwa na nesi mmoja akatoka.
"Kaka huyu dada namfahamu, nafikiri anafanya kazi Bugando, au siyo?" Aliuliza.
"Hapana nafikiri umemfananisha," Mike alificha.
"Si anafunga ndoa hivi karibuni, maana kuna rafiki yangu wanafanya naye kazi Bugando aliniletea kitambaa cha sare kwa ajili ya harusi ya dada huyu na tayari nimeshashona, siyo huyu kweli?" Aliendelea kuuliza.
"Nafikiri umemfananisha," Mike alijibu harakaharaka.
Maswali ya dada yule yalimuumiza sana Mike na hakutaka kabisa yaendelee. Alijua ni lazima yangefika mahali pa kuulizwa sababu ya Beatrice kuamua kufanya hivyo, kitu ambacho Mike hakuwa tayari kukiongelea.
"Samahani dada kwani huko ndani kunaendelea nini?" Mike aliuliza kwa sauti iliyojaa wasiwasi.
"Anaendelea vizuri ila mapigo yake yapo chini mno, tumejaribu kuyainua kidogo lakini bado!"
"Je, anapumua?"
"Anatumia mashine ya oksijeni!"
"Lakini atapona kweli sista?"
"Usiwe na wasiwasi, tuendelee kumwomba Mungu."
Kauli hiyo ya nesi ilimtia Mike hofu zaidi, nesi alipoondoka Mike alianza kusali sala ya “Baba Yetu Uliye Mbinguni!” Alisali sala hiyo mara nyingi mno akimwomba Mungu ayanusuru maisha ya Beatrice.
Mwisho wa sala yake alisema: “Ee Mungu unaijua nia yangu, mimi nina virusi lakini Beatrice hana, nimejaribu kila niwezalo kuokoa maisha yake lakini Beatrice hanielewi, Ee Mungu wangu, kosa langu mimi ni lipi? Baba nipe njia iliyo njema ya kuepuka tatizo hili!"
Mike aliendelea kusali huku machozi yakimtoka.
Akiwa katikati ya mawazo, mara mlango wa chumba cha wagonjwa mahututi ulifunguliwa tena.
Mike alisimama wakati huo machozi yakimtoka.
"Sista vipi? Kuna nini? Tafadhali niambie ukweli!" Mike aliuliza maswali mengi kabla hajajibiwa swali moja.
"Hakuna tatizo ila naomba uingie ndani maana hapo nje kuna mbu wengi sana, njoo tu huku ndani ukae karibu na mgonjwa wako!"
"Asante sana sista,” alisema Mike na kabla hajaingia alikumbuka kitu:
"Sista kuna sehemu naweza kupiga simu hapa?'
"Unataka kupiga simu wapi?"
"Nyumbani kwao Beatrice kwani hawana habari juu ya haya yanayotokea."
"Hawana habari?"
"Ndiyo!"
"Basi ingia humu ndani nitakupatia simu."
Mike aliingia ndani na kwenda moja kwa moja hadi ofisini kwa nesi na kupewa simu. Alipiga simu ya nyumbani kwa Samson ambapo simu iliita kwa muda mrefu sana bila kupokewa. Hakuwa na haraka kwa kuwa alijua kabisa kuwa kwa wakati ule lazima walikuwa wamelala. Baada ya kungoja kwa muda wa dakika tatu simu ilipokewa.
"Hallow! Hallow nani anaongea?" Ilikuwa ni sauti ya Samson.
"Ni mimi Mike."
"Vipi mbona usiku hivi simu?"
"Nipo Hospitali ya Sekou Toure, Beatrice amelazwa"
"Amelazwa anaumwa nini?"
"Ah! Alitaka kutimiza alichokiahidi na sijui kama atapona. Kwa kweli inaniuma sana na ninahitaji msaada wenu."
"Kweli?"
"Ndiyo."
"La, tumejaribu sana kumtafuta na hata tukapiga simu nyumbani kwako lakini ilikuwa haipokewi!”
"Nafikiri ni wakati huo ndio nilikuwa nahangaika hospitali, nilikuwa nimechanganyikiwa mno!”
"Ok! Tunakuja sasa hivi."
Dakika kumi baadaye Samson na Maggie walisimamisha gari getini mbele ya Hospitali ya Sekou Toure.
"Mzee, samahani unaweza kutueleza ni wapi ilipo wodi ya wagonjwa mahututi?" Walimuuliza mlinzi waliyemkuta getini.
"Zungukeni upande wa pili kuna chumba kimeandikwa ICU," aliwafahamisha.
Walizunguka kama walivyoelezwa, haikuwa kazi kubwa kukiona chumba hicho. Walibonyeza kengele iliyokuwa mlangoni na mlango ukafunguliwa.
"Karibuni!" Ilikuwa ni sauti ya nesi wa zamu.
"Asante sana! Mimi naitwa Samson na huyu ni mke wangu anaitwa Maggie, tunaomba utusaidie kumwona ndugu yetu amelazwa hapa wodini."
"Hivi sasa siruhusiwi kabisa kuingiza mtu wodini, hata hivyo nitawasaidia , ndugu yenu ni Beatrice?"
"Ndiyo, anaendeleaje?" Aliuliza Maggie.
"Hali yake siyo mbaya ingawa haongei, haya ingieni mmuone!"
Samson na Maggie waliingia chumbani na moja kwa moja walikwenda hadi kitandani ambako walimkuta Mike alipowaona tu alianza kulia tena.
"Mike wewe ni mwanamume, jikaze," Samson alimsihi.
"Nashindwa Samson, Beatrice amefanya kitu kibaya sana kama akifa mimi nitajisikia vibaya mno maisha yangu yote. I will feel guilty for the rest of my life” (Nitajisikia mwenye hatia maisha yangu yote).
"Nyamaza shemeji, Beatrice hawezi kufa," Maggie alimpoza Mike.
Maggie aliinama na kumwangalia Beatrice pale kitandani, alipomwona Beatrice anatupa shingo yake huku na kule naye pia alishindwa kuvumilia akaanza kulia huku akisema maneno ya Kihaya: "Omwisiki ogu mufela nayenda kushasa emitima yaitu busha." (Msichana huyu ni mjinga sana anataka kututia huzuni ya bure).
Wote walisimama wakiwa wamekizunguka kitanda bila kujua la kufanya. Chupa za maji ziliendelea kuingia katika mishipa ya Beatrice. Mdomoni alikuwa amefungwa mashine ya kusaidia kupumua.
"Samson kweli Beatrice atapona?" Mike aliendelea kuuliza.
"Usiwe na wasiwasi atapona tu," Samson alimliwaza.
"Heri ningemuoa."
Saa tisa usiku Samson na Maggie walipitiwa na usingizi lakini Mike alibaki amesimama pembeni mwa kitanda akimwangalia Beatrice. Hakuwa hata na lepe la usingizi. Yote hayo yalitokana na kutaka kufahamu maendeleo yote ya mpenzi wake.
Ilipotimia saa kumi na moja alfajiri wakati muadhini anaadhini, kwa mbali Mike alimwona Beatrice akifumbua macho. Aliwaangalia Samson na Maggie wakiwa wamelala huku wameegemea meza, akawatingisha.
"Amkeni, Beatrice kafumbua macho! Kafumbua macho! Kafumbua macho!” Mike alisema kwa sauti kama mtu aliyepagawa, alikuwa na furaha mno moyoni mwake.
Samson na Maggie waliinuka na kukimbilia kitandani ambako walimkuta Beatrice kweli kafumbua macho na kuyapepesa akiangalia darini.
"Lihimidiwe jina la Mungu!" Samson alisema na wote wakapiga magoti kumshukuru Mungu. Walipomaliza walisimama na kuendelea kuangalia maendeleo yake.
Je nini kitaendelea?


No comments