Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA UHAI WANGU - 8

MUENDELEZO Jumapili asubuhi Mike aliamua kwenda kusali, lengo lake likiwa kutubu dhambi zake zote kwa vile alijua hakuwa tena na mais...

Image result for siku za mwisho za uhai wangu 7

MUENDELEZO
Jumapili asubuhi Mike aliamua kwenda kusali, lengo lake likiwa kutubu dhambi zake zote kwa vile alijua hakuwa tena na maisha marefu mbele yake. Hakujua dhambi alizokuwa nazo lakini aliamua kwenda kutubu tu.
Kanisani Mike alikaa kiti cha nyuma kabisa.
Kama dakika kumi baada ya yeye kuingia akiwa katikati ya sala alisikia sauti ya viatu vikigonga sakafuni kwa nguvu. Alipogeuga nyuma macho yake yaligongana na ya Beatrice ambaye alikuwa akiingia kanisani.
Beatrice alionekana kakonda mno na mwenye huzuni kubwa, alipita moja kwa moja hadi kwenye kiti kilichokuwepo mbele ya Mike na baada ya misa waumini wote walitoka nje ambako Beatrice na Mike walikutana.
"Mike sikiliza hivi umechoka kuniona duniani au?"
"Hapana Beatrice, nakupenda mno na nisingependa kukupoteza, ndiyo maana sitaki kukuambukiza virusi! Kwa nini hutaki kunielewa Bite?"
"Mike kumbuka mwisho ni saa 72 ni leo saa tatu usiku, kama muda huo utafika bila kunitaarifu kuwa umebadili msimamo wako utanikuta naning'inia mtini unasikia?”
Baada ya kusema hayo Beatrice alianza kutoa machozi na kuondoka bila kuaga!
Mike alibaki kimya, kwa upande mmoja maneno ya Maggie kuwa Beatrice asingejiua yaliendelea kumtia nguvu lakini alipojaribu kufikiria upande mwingine, hasa kutokana na hali aliyokuwa nayo Beatrice pale kanisani, Mike alianza kuhisi kuwa yawezekana kabisa Beatrice angefanya kweli.
Alipofika nyumbani Mike akiwa mwenye mawazo mengi, alijitupa kitandani na kulala. Aligutuka usingizini saa tatu kasoro dakika kumi! Alikuwa amelala kwa karibu saa kumi mfululizo tangu atoke kanisani.
Ghafla alikumbuka kitu akilini mwake, kengele ya hatari iligonga kichwani mwake, zilikuwa zimebaki dakika kumi tu Beatrice ajinyonge kama kweli nia yake ilikuwa hiyo.
***
Mike aliinua simu na kupiga nyumbani kwa Samson, kuulizia kama kweli Beatrice alikuwepo.
"Ngoja nimwangalie chumbani mwake," Maggie aliongea bila wasiwasi wowote.
"Beatrice hayupo ndani lakini usiwe na wasiwasi wowote Mike!" Maggie alimpoza.
Maneno yale ya Maggie yalimtia Mike wasiwasi, alitoka nje na kuingia ndani ya gari kuelekea Capri Point, dakika saba tu zilikuwa zimebaki kabla ya kwisha kwa muda aliotoa Beatrice.
Mike aliendesha gari huku akimwomba Mungu njiani kusiwe na msongamano wa magari ambao ungemkwamisha kufika Capri Point kabla ya saa tatu kamili.
Alipokuwa akiingia barabara ya Nyerere, askari mmoja wa usalama barabarani alimsimamisha lakini Mike alipuuzia na kuendelea na safari yake.
"Tutajua kesho," Mike alijisemea baada ya kumpita askari huyo.
Alipofika eneo la kituo cha mafuta cha Jamhuri, karibu na jengo la Benki ya Taifa ya Biashara alikutana na msusuru mrefu wa magari uliosababishwa na ajali mbaya iliyotokea eneo hilo!
Alipoangalia saa yake ilionyesha kuwa zilikuwa zimebaki dakika tano tu, akaamua kuliweka gari pembeni akatoka na kukimbia hadi mtaa wa pili, alikochukua teksi na kumwamuru dereva aendeshe kwa mwendo wa kasi kuelekea Capri Point.
***
Walipofika maeneno ya bustani ya CCM, makao makuu dereva aliona kitu na kumgutua Mike.
"Ona yule dada anapanda kwenye mti usiku huu sijui anatafuta nini?”
"Yuko wapi?"
"Pale kwenye mti mkubwa!" Dereva alimwonyesha tena huku akipunguza mwendo.
"Achana naye, wewe ongeza mwendo kuna kitu cha muhimu sana tunawahi!" Dereva akabadilisha gia na kuweka namba nne, kisha kukanyaga mafuta ya kutosha.
Alipoangalia saa yake ilimwonyesha saa 2:58 na ghafla wazo lilimjia.
"Mungu wangu yule dada anaweza kuwa Beatrice sijui nirudi nikamwangalie au sijui niende tu?" Mike alijiuliza na kujikuta yuko njia panda.
"Geuza gariii!" Mike alimwamuru dereva wa teksi na bila ubishi, dereva alipiga “norinda” gari likatimua vumbi na kukata kona.
Walirudi mahali pale walipomwona yule msichana, dereva wa teksi alifanya yote hayo bila kujua linaloendelea, alifanya hivyo kutii amri ya tajiri wake.
Walipoukaribia ule mti ilikuwa inatimia saa 2:59:58! Zilikuwa zimebaki sekunde mbili tu kufika saa tatu. Mike alikwishakata tamaa ya kuyaokoa maisha ya Beatrice tena.
Alipofika pale chini ya mti yule msichana alijiachia na kamba ikamkaba shingoni! Alipoviangalia vizuri viatu alivyovaa msichana yule ALIVIFAHAMU! Vilikuwa ni viatu ambavyo alimnunulia Beatrice kama zawadi kutoka Uingereza.
Baada ya kugundua kuwa aliyekuwa akijinyonga ni Beatrice, Mike alipiga kelele kama mwendawazimu Beatrice don't kill yourself! (Beatrice usijiue).
Aliushukuru uamuzi wake wa kuamua kugeuza gari.
Tayari Beatrice alikuwa akining'inia mtini! Bila kuchelewa Mike aliikamata miguu ya Beatrice na kuisukuma juu ili Beatrice asizidi kukabwa zaidi. Wakati akifanya hivyo alimwita dereva aje amsaidie.
"Una kisu hapo karibu?" Alimuuliza dereva alipomkaribia.
"Ndiyo lakini kipo ndani ya gari."
"Kilete upesi, nisaidie kuikata kamba shingoni mwake."
Dereva alikimbia haraka kwenda kwenye gari na kuchukua kisu. Aliporudi alipanda harakaharaka mtini na kuikata ile kamba! Beatrice akaanguka chini kama mzigo.
Mike alipomchunguza Beatrice kwa harakaharaka kifuani aligundua alikuwa hapumui na alipomgusa upande wa moyo alihisi kutopiga.
"Dereva hebu mshike na wewe kifuani, nashindwa kugundua vizuri kama moyo wake unapiga au umesimama."
Dereva aliushika moyo wa Beatrice.
"Hata mimi siusikii ukipiga." Mike alizidi kuchanganyikiwa.
"Sasa wewe mpigepige kifuani upande wa moyo na mimi nimpulizie pumzi mdomoni labda ataamka," Mike alisema kwa hofu kubwa.
"Kwani huyu msichana ni nani yako?" yule dereva aliuliza.
"Okoa maisha kwanza tutaongea baadaye!"
Mike alianza kumpulizia Beatrice pumzi ya uhai mdomoni na dereva akawa anaupigapiga moyo wa Beatrice ili kuushtua lakini pamoja na juhudi zote hizo Beatrice hakuamka. Alionekana kama mtu aliyekwishapoteza uhai wake.
Jambo hilo lilimuuma sana Mike, alipofikiria kifo cha Beatrice alisikia uchungu sana moyoni mwake na machozi yakaanza kumdondoka.
"Ni heri ningekubali kumwoa," Mike aliwaza huku akiendelea kulia, ndani ya nafsi ya alijilaumu sana kwa kusababisha kifo cha mwanamke aliyempenda.
"Dereva sogeza gari tujaribu kumpeleka hospitali."
"Hospitali gani?"
"Sekou Toure!"
Dereva alilisogeza gari na wote wakampakia na kuondoka kuelekea Isamilo, mahali ilipo hospitali ya Sekou Toure.
Walipofika hospitali wote waliteremka garini na kumbeba Beatrice hadi mapokezi.
"Huyu dada si alikuwa hapa juzi tu?" Muuguzi mmoja pale mapokezi aliuliza baada ya kuziona bendeji alizokuwa nazo Beatrice usoni.
"Ndiye."
"Imekuwaje?"
Mike alipata kigugumizi kulijibu swali hilo lakini alipogundua kuwa ilikuwa ni lazima kusema ukweli ili aokoe maisha ya mpenzi wake ilibidi atoe jibu.
"Alikuwa akijaribu kujinyonga."
"Unasemaje?" Aliuliza yule nesi kwa mshangao na Mike akarudia tena kutoa jibu.
"Kwa sababu gani?"
Swali hilo lilifuatiwa na kimya kikubwa.
Bila kuchelewa, Beatrice alikimbizwa chumba cha wagonjwa mahututi ambako alilazwa na kutundikiwa chupa ya maji ya Normal Saline ambayo yalikwenda kwa kasi ili kunyanyua mapigo yake yaliyokuwa chini sana.
Pia, daktari aliagiza awekewe mashine ya hewa ya oksijeni ili kumsaidia kupumua. Alidai kama kusingefanyika juhudi za haraka, maisha ya Beatrice yangepotea kwa kuwa mapafu na moyo wake yalikuwa hayafanyi kazi vizuri.
Je nini kitaendelea?

USISAHAU CLICK SUBSCRIBES  KUFOLLOW SOCIAL NETWORKS
COMMENT HAPO CHINI 

No comments