Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA ZA UHAI WANGU 7

MUENDELEZO Wakati Mike anateremka kuelekea majini, Beatrice alikuwa akivuja damu nyingi usoni kutokana na jeraha kubwa alilolipata baad...

Image result for siku za mwisho za uhai wangu 7

MUENDELEZO
Wakati Mike anateremka kuelekea majini, Beatrice alikuwa akivuja damu nyingi usoni kutokana na jeraha kubwa alilolipata baada ya kujigonga kwenye mwamba. Aliogelea taratibu na kukaa juu ya jiwe nyuma ya kilima na kuendelea kulia.
Aliujutia muda alioupoteza kumsubiri Mike ambaye tayari alikuwa amemtelekeza na kwa kitendo kile aliwaona wanaume wote duniani ni wanyama.
Wakati Mike akiwa amekata tamaa kabisa, alitupa macho kwa chini na kumwona Beatrice amekaa juu ya jiwe, huku akitokwa na machozi. Alimfuata na kumbeba mgongoni na kupanda naye hadi nchi kavu ambako hakuna mamba wala mdudu yeyote aliyewagusa!
"Beatrice, imekuwaje mpenzi?"
"Ni heri nife Mike! Nimepoteza muda na vitu vingi sana kwa ajili yako, huwezi kunifanyia unyama huu na ukategemea niendelee kuishi, huu ni ukatili Mike. Mike huna hata huruma? Huwezi kunifikiria?"
"Beatrice amini nakupenda, na I am doing all these to protect you (na ninafanya hayo yote kukulinda wewe) kwa sababu sitaki kuua kiumbe asiye na hatia.”
"Mike ujanja unaoutumia ni wa kizamani sana, ni heri ungeniambia tu ukweli na ninakuambia Mike usiponioa najiua, sihitaji kuishi tena. Hebu fikiria watu wote hivi sasa wanajiandaa kwa ajili ya harusi yetu, nitawaeleza nini mimi? Sura yangu nitaificha wapi Mike!" Beatrice alisema huku akilia.
Damu kwenye jeraha usoni mwake ilizidi kumwangika!
"Beatrice twende nikupeleke hospitali!" Mike alisema.
"Sitaki kwenda hospitali, niache nife kwani hata nikifa itakuuma nini wewe?" Beatrice alimaka kwa hasira.
Mike alivua shati lake na kumfunga Beatrice usoni ili kuzuia damu isiendelee kutoka na alizidi kumbembeleza akubali kupelekwa hospitali na mwishowe alikubali.
Walipanda boti na kurudi Mwanza mjini. Mike akiwa kifua wazi! Ilikuwa aibu kwa mtu mwenye madaraka kama yake lakini hakujali.
Ng'ambo walipanda gari na kuelekea hospitali ambapo Mike alipita eneo la Makoroboi kwenye maduka ya Wachaga na kununua shati jipya akavaa.
Alimpeleka Beatrice hadi hospitali ya Sekou Toure ambako alishonwa nyuzi kumi na mbili usoni na kuruhusiwa kurudi nyumbani kwa sababu alikuwa hakuumia kiungo kingine cha mwili. Bahati nzuri kina cha maji mahali alipoangukia kilikuwa kirefu.
Njiani wakati wakirudi nyumbani Beatrice aliendelea kulia na Mike alizidi kumbembeleza akimweleza umuhimu wa mambo aliyoyaandika katika barua lakini bado Beatrice hakutaka kuelewa.
Alizidi kusisitiza waoane kwani aliyaona majibu yale ni ya bandia ili aachwe kijanja!
Walipofika Capri Point dada yake Beatrice alishangazwa na bendeji alizokuwa nazo mdogo wake usoni, wakati huohuo akilia.
"Mike vipi tena, leo mmepigana?" Maggie aliuliza.
"Hapana, Maggie, ila ni habari ndefu sana!" Mike alijibu.
"Yaani Mike umeamua kunifanyia hivyo, sawa tu!" Beatrice alisema.
"Mike vipi, mbona siwaelewi?" Alizidi kuhoji Maggie.
Wakati wakiendelea na hali hiyo mara shemeji yake Beatrice, mume wa Maggie, aliegesha gari nyumbani.
"Ndugu zangu vipi mbona bendeji kichwani, mnanitisha, kuna nini tena Maggie?" alimuuliza mke wake.
"Hata mimi ndio nauliza, sababu ndio kwanza wamefika, halafu naona kama wote walikuwa wanalia vile."
"Mike wewe ni mwanamume, hebu njoo ndani utueleze kilichotokea," Samson alisema.
"Ni habari ndefu jamani ambayo hata ninyi nikiwasimulia itakuwa ngumu sana kuiamini lakini ndivyo ilivyo," Mike alisema na baadaye akawasimulia.
"Beatrice aliponipeleka Bukoba kwa wazazi wake walinikubalia nimwoe lakini walishauri kwanza tupime UKIMWI kabla ya ndoa yetu. Tuliporudi Mwanza vikao vya harusi vilianza kufanyika, hatukupimwa mara tu baada ya kufika hapa kutoka Bukoba kwa sababu tulijiamini mno...!" Mike alisema wote wakiwa kimya. Kwikwi za kilio cha Beatrice ndizo zilizosikika.
Baadaye Mike aliendelea: "Tulijiamini mno kwa sababu mpaka wakati huu mimi binafsi sijawahi kukutana na mwanamke kimwili, mnaweza kuamini au msiamini lakini huo ndio ukweli.
Hilo hata Beatrice mwenyewe analijua na mimi naamini yeye pia hajawahi kufanya hivyo na wote tulikuwa tukisubiri siku ya ndoa yetu ili tufanye kitendo hicho. Siku chache zilizopita mzee Rugakingira alinipigia simu na kunikumbusha juu ya suala la kupimwa UKIMWI.
Ili kumridhisha tuliamua kwenda kupimwa na majibu ya kwanza yalipotoka yalionyesha mimi ni Positive na Beatrice ni Negative! Sikuyaamini majibu hayo, nilijua wananidanganya au wamekosea kupima. Ikabidi nirudie tena kupimwa huko Medical Research kwa mtu ninayemwamini zaidi. Majibu yalipotoka yalikuwa vilevile, nilikuwa HIV Positive.
Nilichanganyikiwa mno! Sikuwa na la kufanya ilibidi nilazimike kuyaamini majibu hayo, majibu yenyewe ni haya hapa!" Mike akaingiza mkono mfukoni na kutoa ile barua na majibu, akamkabidhi Maggie ambaye naye machozi yalikuwa yakimlengalenga.
"Baada ya kupata majibu hayo nilijaribu kumfikiria Beatrice, kwa bahati nzuri mimi na yeye hatujawahi kukutana kimwili hata siku moja kwa sababu ninampenda na sitegemei kama penzi la kweli linaweza kuua, nimeamua kutofunga ndoa hii!"
Mike aliingiza mkono mfukoni akatoa kitambaa na kuanza kujifuta machozi yaliyokuwa yakimlengalenga, halafu aliendelea, "Nayafanya yote haya kwa sababu nampenda Beatrice, sitaki kuua kiumbe kisicho na hatia. Beatrice ni msichana mzuri sana, ni bora nimpe nafasi ya kuolewa na mtu mwingine, kwangu mimi hili naona ndio penzi la kweli!
Nilishindwa nimweleze vipi Beatrice juu ya jambo hili, ndiyo maana nikaamua nimwandikie barua hiyo lakini alipoisoma alianza kunilalamikia kuwa nataka kumwacha kijanja na kabla sijakaa sawa alijirusha kutoka pangoni kule kisiwa cha Saa Nane. Akapasuka juu ya jicho na hivi sasa kashonwa nyuzi kumi na mbili!!” Mike alisema akijifuta machozi.
"Jamani nisaidieni, nachanganyikiwa, nifanye nini, najaribu kumwokoa Beatrice lakini hataki kuokolewa!" Mike alimaliza na kwikwi ya kulia ikamkaba, akalia kwa sauti. Samson alimsogelea na kumwekea mkono begani.
"Pole Mike!" alimliwaza.
"Beatrice!" Maggie aliita.
"Bee!"
"Unamsikia mwenzio?"
"Ndiyo, lakini ni mwongo dada, ameamua kuniacha sababu amepata umaarufu sana siku hizi lakini ukumbuke mimi na yeye tulikoanzia! Amewahonga madaktari ili aonekane ana virusi!"
"Beatrice usiwe mpumbavu, hawezi kufanya hivyo, wewe huoni ni mihuri ya Bugando na Medical Research?""Dada mimi sitaki naomba uniachie maisha yangu mwenyewe, ninachotaka ni kuolewa!"
"Beatrice una akili wewe? Utakufa!"
"Acha nife Maggie, hata wewe pia utakufa, ni lazima ujue mwisho wa maisha ya binadamu ni kifo na kumbukeni msipokufa kwa UKIMWI mtakufa na malaria, kama si malaria, kifua kikuu, kama si kifua kikuu ni homa ya matumbo lakini mwisho wa kila mwanadamu ni kifo. Vitabu vitakatatifu vinasema kila nafsi ni lazima ionje mauti!" Beatrice alimaliza na kuanza kulia tena.
Walijaribu huku na kule kumbeleleza lakini hakukubali, msimamo wake ulibaki palepale kuwa ni lazima Mike amwoe.
Msimamo huo uliwashangaza wote na ikabidi Maggie amshauri Mike ashikilie msimamo wake ili kuyaokoa maisha ya mdogo wake.
"Dada wewe ndiye unamshauri Mike hivyo, siyo? Sasa mimi natoa saa 72! Hivi sasa ni saa tatu, ikifika Jumapili saa tatu usiku ni lazima Mike awe amebadilisha msimamo wake, vinginevyo najinyonga. Kama hamuamini basi subirini!"
Baada ya kusema maneno hayo Beatrice alinyanyuka na kukimbilia chumbani kwake na kujifungia kwa ndani.
"Mike sikiliza sisi hapa tumeshajua hakuna harusi tena, wewe usiyafuate maneno ya huyu chizi. Umejaribu kumsaidia vya kutosha lakini hataki kuelewa. Binafsi nakushukuru sana kwa moyo wako wa upendo," Maggie alisema.
"Sasa umekwisha jaribu kuchunguza ni wapi tatizo hilo ulilipata?" Samson aliuliza.
"Kwa kweli sijui ila nina wasiwasi sana na damu niliyoongezewa Copenhagen wakati ule nilipofanyiwa upasuaji. Unajua wakati huo utaratibu wa kupima damu kama ina virusi kabla mtu hajaongezewa haukuwepo. Hilo ndilo linanitia wasiwasi na nina hakika ni wakati huo ndipo niliambukizwa, amini usiamini Samson, sijawahi kukutana na mwanamke kimwili."
Saa nne usiku Mike alisindikizwa hadi nje ambako alichukua gari lake na kurejea nyumbani kwake Bugando.
***
Siku iliyofuata Mike alikwenda kazini kama kawaida lakini kazi zilimshinda, ikamlazimu aondoke kazini majira ya saa tano kurejea nyumbani. Aliamua apitie nyumbani kwa wazazi wake kuwasalimia na pia kuwaeleza juu ya tatizo lake.
Alipofika nyumbani alikuta shamsharamsha za maandalizi ya harusi. Ilionekana kabisa kuwa maandalizi yalikuwa yakifanyika harakaharaka. Pembeni ya nyumba yao kulikuwa na ng'ombe kumi na mmoja walioandaliwa kwa ajili ya harusi yake.
Hali aliyoikuta nyumbani kwao ilimpa huzuni kubwa. Alishindwa kuelewa angewaeleza nini watu wote waliokuwa wamejiandaa kwa harusi yake.
Mike alisikia uchungu sana moyoni kwa jinsi alivyowaona akinamama wakichambua mchele na wengine wakiimba nyimbo mbalimbali kwa furaha. Walikuwa hawajui yaliyokuwa yakimsibu moyoni mwake.
Baadaye mama yake aliyekuwa jikoni alitokea sebuleni ambako Mike alikuwa amekaa.
"Mwanangu Mike kwa nini huwezi kuchangamka wakati hii ni harusi yako? Kwa nini una huzuni kiasi hicho? Unanikwaza mimi mama yako!" Alisema mama yake.
Machozi yalitaka kumtoka Mike lakini alijizuia kwa furaha aliyoionyesha mama yake, alishindwa kusema kilichokuwa kikimsumbua moyoni mwake, ikabidi akichimbie moyoni.
"Mike mwanangu unaumwa baba?" Mama yake aliuliza.
"Ndiyo mama!" Alijibu.
"Unaumwa nini mwanangu?" Mama aliuliza kwa wasiwasi.
"Mafua mama!" Alijibu harakaharaka.
"Sasa ni kwa nini usinywe vidonge vya Contac au Piriton mwanangu, unaendekeza ugonjwa wakati siku zenyewe zimebaki chache?" mama yake alionekana kutofahamu kitu.
Hapo Mike alishindwa kujizuia ikabidi machozi yamtoke, akachukua kitambaa na kujifuta kabla mama yake hajagundua.
"Nimepanga kununua Contac nikifika mjini mama."
Alipotoka nyumbani kwao alikwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwake na kujitupa kitandani. Hakuchukua muda mrefu akapitiwa na usingizi. Kitendo cha kutolala kwa siku mbili mfululizo kilisababisha alale usingizi mzito. Hakuzinduka hadi saa tano usiku. Baada ya hapo hakulala tena mpaka asubuhi. Siku hiyo pia hakwenda kazini, aliamua kushinda nyumbani, akiwaza na kuwazua matatizo yaliyokuwa yakimsibu. Jioni alimpigia simu Beatrice na kuongea naye, aliendelea kusisitiza msimamo wake.
"Mike kumbuka zikipita saa 72 tu nisilaumiwe, si wewe unajifanya kumsikiliza Maggie kuliko mimi?" Alipomaliza kusema hayo akakata simu.
Mike alizidi kuchanganyikiwa, hakujua la kufanya, tatizo la Beatrice tayari kwake lilikwishakuwa kubwa kuliko hata tatizo alilokuwa nalo yeye. Alijaribu kufikiria nini afanye ili kumwelewesha juu ya nia nzuri aliyokuwa nayo.
Mike alikosa njia kwa kuwa tayari Beatrice alikwishajenga hoja akilini mwake kuwa Mike alifanya hivyo ili amtelekeze. Kila alipofikiria walikotoka na Beatrice tangu enzi za Nsumba, alichanganyikiwa, alishindwa kuelewa ni nini kilikuwa kikitokea katika maisha yake.
Pamoja na hayo yote hakutaka kabisa kumwoa Beatrice kwa sababu kwa kufanya hivyo ilikuwa ni sawa na kumchinja au kumtilia sumu kwenye chakula.
Je nini kitaendelea?
Tuonane kesho.
Unaweza kupongeza, kunishauri chochote kwa comment yako na mimi kukujibu au kukushukuru.

No comments