Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

HADITHI: SIKU ZA UHAI WANGU 2

MWISHO ZA UHAI WANGU 2 Mvulana aliyekuwa na uwezo mkubwa darasani ambaye alikuwa akisoma katika Shule ya Wavulana ya Nsumba ya jijini Mwa...

MWISHO ZA UHAI WANGU 2
Mvulana aliyekuwa na uwezo mkubwa darasani ambaye alikuwa akisoma katika Shule ya Wavulana ya Nsumba ya jijini Mwanza, Mike Martin anajikuta akiwavutia wasichana wengi hasa wa Shule ya Wasichana ya Ngaza.
Anajikuta akipokea barua nyingi kutoka kwa wasichana hao lakini kitu cha ajabu, hakutaka kuwa na msichana yeyote yule. Mbali na uwezo wake mkubwa darasani, Mike alikuwa na uwezo mkubwa wa kucheza muziki kitu kilichowafanya wanafunzi kumuita jina la Double Mhuku wakimfananisha na mwanamuziki Michael Jackson.
Upande wa pili, msichana mpole na mtaratibu ambaye naye hakuwahi kukutana na mwanaume kimwili, ambaye alikuwa akisoma katika SHule ya Wasichana ya Ngaza anajikuta kuvutiwa na MIke, moyo wake unaweweseka, mapnzi mazito yanaugubika moyo wake.
Anaogopa kwa kuwa hajawahi kuzungumzia mapenzi na mvulana yeyote yule. Anapoona ameshindwa kabisa kuongea na Mike, anajukuta akijifariji kwa kusema kwamba milima haikutani ila binadamu hukutana, ipo siku atakutana tena na Mike.
SONGA NAYO...
Ilikuwa ni Januari 27, 1976 siku ambayo wanafunzi mia moja wa shule ya Nganza walialikwa kwenda kucheza disko na wanafunzi wa shule ya wavulana ya Nsumba katika sherehe ya kuwakaribisha wanafunzi wa kidato cha kwanza shuleni hapo iliyojulikana kwa jina la “Welcome Form One!” Kiranja mkuu wa shule ya Nganza, Neema Lucas, alipopewa barua hiyo na mwalimu wa zamu alifanya hima kuwatangazia wanafunzi wenzake na kuwaomba waliopenda kwenda Nsumba wajiandikishe mapema.
Beatrice aliiona nafasi ile kama bahati ya mtende na alikuwa mtu wa sita kujiandikisha. Lengo lake halikuwa kucheza muziki bali kuonana na Mike Martin, mwanaume aliyetokea kuunyanyasa moyo wake kwa nguvu zote.
Kitendo cha Beatrice kujiorodhesha kati ya wasichana waliotaka kwenda Nsumba kilizusha mjadala mkali kati ya wasichana wa Nganza. Beatrice, ambaye siku zote alionekana mlokole, aliwafanya wengi kujiuliza imekuwaje hata akaamua kwenda Nsumba kucheza disko siku hiyo? Wengi walihofu huenda Beatrice naye alikuwa ameanza kuangukia dhambini.
“Hata wewe Beatrice? Ya leo kali!” mwanafunzi mmoja alimuuliza Beatrice baada ya kulisoma jina lake ubaoni.
“Ni lazima niende, siendi kucheza bali nawapelekea watu habari njema! Bila kuwafuata kwenye kumbi zao za starehe wataupataje wokovu? Mbona Kristo alikula na watoza ushuru?” Beatrice hakuwa na njia yoyote ya kujitetea zaidi ya kutumia Biblia hiyohiyo ingawa lengo lake lilikuwa ni kumfuata Mike.
***
Wakati wasichana kutoka Ngaza wakiwasili katika viwanja vya Nsumba, Mike alikuwa bwenini akimalizia kufanya mazoezi ya kucheza shoo ya muziki wa “Thriller” wa Michael Jackson uliokuwa umepangwa kutumika katika onyesho siku hiyo. Pamoja na kuwepo bwenini katika mazoezi makali na ya mwisho alifanikiwa kuliona lori lililokuwa limewachukua wanafunzi wa Nganza likiingia shuleni kwao.
Kitu cha kwanza ambacho wasichana hao walifanya baada ya kuteremka kutoka kwenye lori lililowaleta ni kuuliza mahali alipokuwepo Mike. Jambo hilo lilimkera sana Beatrice, alihisi nafasi yake ya kukutana na Mike ilikuwa finyu.
Muda wa kuanza kwa sherehe hiyo ulipotimu, wanafunzi wa vidato vyote walifurika katika ukumbi wa starehe wa shule ya Nsumba na sherehe ikaanza mara moja.
Macho ya wanafunzi wa Nganza yalizunguka huku na kule ukumbini yakimsaka Mike bila mafanikio. Mike alikuwa bado yuko bwenini akivaa nguo zake za kung’ara zilizomfanya afanane kabisa na Michael Jackson.
Majira ya saa sita usiku, wakati sherehe ikiwa imepamba moto, mshereheshaji au MC kwa Kiingereza, Zablon Julius, aliyekuwa kiranja mkuu wa shule ya Nsumba, aliomba muziki usimamishwe na kuwataka wanafunzi wote wakae vitini na kuacha ukumbi wazi. Muziki uliposimamishwa hakupoteza muda, aliongea kwa sauti ya juu.
“Jamani naomba mkae kwenye viti vyenu mtulie. Hivi sasa ni kipindi cha onyesho maalumu, Show time na tunamkaribisha, The Tanzanian Michael Jackson au Double M aje kutuonyesha show ya wimbo wa “Thriller” ulioimbwa na Michael Jackson.”
Alipomaliza tu kusema hayo ukumbi wote ulipiga mayowe kushangilia na taa zikawashwa ili Mike aonekane vizuri.
Beatrice aliyekuwa amekaa nyuma kabisa ya ukumbi akiwa hajacheza hata muziki mmoja tangu disko lianze, alisogea mbele ili apate kumwona vyema mtu aliyekuwa akiusumbua moyo wake kwa kipindi kirefu.
Baada ya kukaribishwa, Mike hakupoteza muda. Aliingia ukumbini, kitu cha kwanza kukifanya kilikuwa ni kuinua mikono yake juu na kutamka kwa sauti ya juu, “Hi everybody?”
Kauli hiyo iliamsha shamrashamra ya aina yake na waliokuwepo ukumbini walizidi kupiga kelele na kushangilia “Cool Mameeeeeen!” kila mtu aliitika.
DJ alianza kuachia wimbo wa “Thriller” taratibu na Mike akaanza kufanya vitu vyake. Hakuna aliyeamini kama kweli Mike angeweza kufanya vitu vikubwa namna ile. Hata wanafunzi wa Nsumba wenyewe siku hiyo walishikwa na butwaa kwa jinsi Mike alivyojinyonganyonga kama hana mifupa mwilini! Wengi wa wanafunzi walisikika wakidai kwamba siku hiyo alicheza makusudi ili kuwazingua wasichana wa Nganza.
Beatrice alishindwa kujizuia. Alitamani sana kuongea na Mike ingawa hakujua kama Mike angeweza kupoteza muda wake kumsikiliza mtu kama yeye. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake alihisi kutumbukia katika dimbwi kubwa la mapenzi ambalo lilionekana dhahiri kuutesa na kuugubika moyo wake.
Alijikuta akitafuta njia ambayo angeweza kuitumia kuwasiliana na Mike lakini bado hakuigundua kwa sababu karibu kila msichana alitaka kuongea naye.
Muziki ulipokaribia kwisha, ghafla Beatrice alipata wazo aliloona linafaa kuufikisha ujumbe. Aliingiza mkono kwenye mfuko wake wa sketi na kutoa kitabu kidogo, akachana kikaratasi na kuchukua kalamu, kisha akaanza kuandika. Alipomaliza alikichukua kile kikaratasi na kukiweka ndani ya noti na kuikunja!
Hakupoteza muda akaondoka moja kwa moja na kwenda katikati ya ukumbi alikokuwa Mike na kumtunza noti ile. Akiwa katikati ya muziki, huku watu wakimshangilia na wasichana wakimzunguka na kumpiga mabusu usoni, Mike aliipokea noti ile na kuiweka mfukoni mwake.
Baada ya onyesho aliondoka moja kwa moja hadi bwenini ambako alibadilisha nguo na kuvaa suti nzuri aliyonunuliwa kama zawadi na baba yake alipofanya vizuri katika mtihani wake na kuingia kidato cha pili!
Kabla hajaondoka bwenini kurudi ukumbini aliikumbuka ile noti aliyotunzwa na msichana wa Nganza. Ilikuwa ni pesa peke yake aliyotunzwa, akainyanyua suruali yake na kuitoa noti hiyo na kuikunjua. La haula! Ndani ya noti ile kulikuwa na kipande cha karatasi! Alikikunjua na kuanza kukisoma. Kilikuwa kimeandikwa kwa mwandiko mzuri sana:
Mike,
Naitwa Beatrice Rugakingira. Nilivutiwa na wewe kwa mara ya kwanza ulipokuja shuleni kwetu kwenye malumbano! Nahisi kukupenda Mike. Ninajua si kitu cha kawaida kwa msichana kuandika barua na kumtaka mvulana kimapenzi, lakini mimi nimeshindwa kuvumilia Mike na imebidi niseme!
Naapa kwamba siyo malaya na sijawahi kukutana na mvulana kimwili maishani mwangu, kitu ambacho unaweza usikiamini.
Naomba tuonane, tuongee kabla sijarudi Nganza. Tafadhali, usinielewe vibaya. Ni moyo wangu ndio unaonisumbua.
Ni mimi
Beatrice.
Barua ile haikumshtua sana Mike, kwani jambo lile lilikuwa la kawaida katika maisha yake. Alipomaliza kuisoma, aliiweka mfukoni na kuondoka tena kuelekea ukumbini. Aliingia ukumbini kwa siri kubwa na kujikita kwenye kiti cha nyuma kabisa.
Aliketi na kuanza kuwaangalia watu walivyokuwa wakicheza muziki. Ghafla, mawazo ya ile barua aliyoisoma yalimjia tena kichwani mwake! Alijaribu kuikumbuka sura ya msichana aliyempa barua ile bila mafanikio yoyote na kujikuta akijiinamia kwa mawazo.
Baada ya Beatrice kuzunguka ukumbini kwa muda mrefu, akimtafuta Mike bila mafanikio yoyote hatimaye alifanikiwa kumfuma akiwa amejificha kwenye giza. Alijongea taratibu mpaka sehemu ile na kusimama nyuma yake kwa takribani dakika tatu, bila kumwita wala kumgusa huku moyo ukimwenda mbio.
Baadaye Mike alihisi moyo ukimwenda mbio, alihisi mtu akimgusa begani! Alipogeuka sura yake iligongana na ya msichana mrembo, mweusi, mwenye ngozi nyororo na sura ya Kinyarwanda. Akamkumbuka kuwa ndiye aliyemtunza noti.
“Hallow habari yako?” Beatrice alimsabahi huku akitabasamu.
“Ni nzuri tu,” Mike aliitika.
“Karibu dada hakuna tatizo,” Mike alijibu.
Beatrice aliona huo ulikuwa wakati mwafaka kwake kuulizia ujumbe wake.
“Naitwa Beatrice Rugakingira, nafikiri ujumbe wangu umeupata?”
“Ah! Ndiyo! Nimeuona. Kumbe ni wewe!” Mike aliijibu kwa upole.
Baada ya mazungumzo ya muda mfupi walitoka ukumbini na kuelekea bustanini. Wakiwa huko Beatrice alimweleza Mike kila kitu kuhusu alivyojisikia mpaka wakati huo. Mike alishindwa kutoa jibu sahihi, kama alimridhia au la.
“Tafadhali Mike nipe ukweli, unanitesa mwenzio!” Beatrice alilalama huku machozi yakimtoka.
Mike alishindwa kumjibu na badala yake alibaki kimya, ameduwaa.
Waliendelea kuwa pamoja, ilipotimu saa tisa na nusu ya usiku Mike na Beatrice walikuwa bado wapo bustanini. Muda wa kuondoka ulipofika wanafunzi wa Nganza walianza kukusanywa kwa safari ya kurudi shuleni kwao. Wanafunzi wote walikuwepo kwenye gari isipokuwa Beatrice. Mwalimu aliyeongozana na wanafunzi kwenda Nsumba aliamuru Beatrice atafutwe haraka iwezekanavyo kabla hawajaondoka.
Baada ya msoko wa hapa na pale wanafunzi wa Nganza walifanikiwa kuwafuma Beatrice na Mike wakiwa wamekumbatiana bustanini. Wanafunzi hao walishangaa kumwona mlokole Beatrice katika hali ile.
Hata hivyo, walichofanya ni kumvuta tu Beatrice na kuondoka naye. Alipofika mbele hatua kama tano Beatrice aligeuka nyuma na kumwangalia Mike.
“Nenda tu, nitakuandikia barua,” Mike alisema wakati akiondoka. Beatrice alimpungia mkono Mike, huo ndio ukawa mwanzo wa Beatrice na Mike kukutana na kupendana.
Wiki moja baadaye Mike alipokea zawadi ya kanda kutoka kwa Beatrice. Kanda ile ilikuwa imerekodiwa sauti ya Beatrice akilia huku akimwomba Mike amhurumie na kukubali kuwa mpenzi wake.
Ilimaliza kwa ujumbe kutoka katika wimbo wa taarab usemao Jamani Mapenzi Yananitatiza ulioimbwa na JKT Taarab.
Kanda hiyo ilimchanganya sana Mike na kwa mara ya kwanza katika maisha yake, alihisi kumpenda msichana kwa dhati. Siku iliyofuata alimwandikia barua kulikubali rasmi ombi lake lakini kwa masharti kwamba penzi hilo liwe la kawaida, siyo linaloshirikisha tendo la ndoa.
Je nini kitaendelea? RNGM blog
Je Mike atakubali kuwa na msichana Beatrice.
Na kama wakiwa pamoja, ahadi ya kutofanya mapenzi itatiizwa?

No comments