Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

HADITHI: SIKU ZA UHAI WANGU

SEHEMU YA KWANZA MIKE MARTIN 1958-1996 (1) ILIKUWA ni alfajiri yenye mawingu mazito angani. Kila mtu alijua mvua ingenyesha siku hiyo k...

SEHEMU YA KWANZA

MIKE MARTIN 1958-1996 (1)
ILIKUWA ni alfajiri yenye mawingu mazito angani. Kila mtu alijua mvua ingenyesha siku hiyo kwani dalili zote za mvua zilikuwepo angani. Waliokuwa wamelala walizidi kujifunika mablanketi vitandani mwao na waliokuwa wameamka walivaa masweta na kuendelea na shughuli zao za kila siku. Ndege wa kila aina walisikika wakilia mitini, jambo lililoashiria kuwa siku mpya ilikuwa imeanza.
Wakati huo Mike Martin alikuwa mwanafunzi wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Nsumba. Alikuwa kijana mkimya, mtaratibu na asiye na makuu katika mambo yake. Akiwa katika umri wa miaka kumi na minane, Mike alikuwa kijana mwenye uwezo mkubwa sana darasani. Alijali na kutilia maanani sana masomo yake.
Zaidi ya hayo, Mike alikuwa na uwezo mkubwa wa kuongea na kuandika kwa lugha ya Kiingereza, jambo lililofanya awe kivutio kikubwa sana miongoni mwa wanafunzi wenzake. Walimu wake walijivunia kuwa na mwanafunzi kama yeye.
Sifa za Mike hazikuishia hapo, alikuwa na sifa nyingine tena ya ziada ambayo ni kucheza muziki. Sio siri, Mike alijua namna ya kuucheza muziki, hasa wa Pop, kiasi kwamba wanafunzi wenzake walimbandika jina la “Double M” au Michael Jackson wa Tanzania!
Sifa za Mike zilitapakaa sana katika shule zote za sekondari mjini Mwanza, hasa katika shule ya Ngaza ambako alikuwa gumzo kwa kila msichana. Kutokana na sifa hizo wasichana wengi walitamani sana kumwona Mike ana kwa ana.
Mara kwa mara alipokea barua, kadi na maua kutoka kwa wasichana mbalimbali asiowafahamu wa shule ya Nganza. Sifa nyingine kubwa aliyokuwa nayo ambayo iliwashangaza hata wanafunzi wenzake ni uhusiano wake na wasichana. Mike hakuwahi kutembelewa na mwanafunzi wa kike kutoka shule nyingine ambaye wanafunzi wenzake wangeweza kuhisi alikuwa mpenzi wake!
Pamoja na kufikisha umri wa miaka kumi na minane alikuwa bado hajakutana na mwanamke kimapenzi. Si kwamba alikuwa na kasoro, ila hakuona umuhimu wa kufanya mawasiliano na wasichana kwa wakati huo. Jambo hilo liliwatesa wasichana wengi waliotamani kuwa na uhusiano naye kimapenzi.
Kijiografia shule za sekondari za Nsumba na Nganza zilikuwa jirani zikiwa zimetenganishwa na kilima kidogo tu katikati. Kwa muda mrefu wanafunzi wa shule hizo walikuwa na uhusiano mzuri wa ujirani mwema.
Wanafunzi wa shule ya Nsumba walipokuwa na sherehe, waliwakaribisha wanafunzi wa shule ya Nganza ambayo ilikuwa ni ya wasichana watupu.
Vilevile, wanafunzi wa Nganza walipokuwa na sherehe waliwaalika wanafunzi wa shule ya Nsumba iliyokuwa ya wavulana watupu, kwenda kucheza nao muziki. Huo ndio uliokuwa uhusiano wa shule hizo mbili.
***
Mara ya kwanza Mike kufika shuleni Nganza ilikuwa Mei 23, 1975. Siku hiyo wanafunzi wa Nsumba walikuwa wamealikwa kwenye malumbano ya hoja ambayo kwa kimombo huitwa “debate.” Yalikuwa ni juu ya Yapi Yalikuwa Maisha Bora kati ya Maisha ya Mjini na ya Vijijini. Malumbano hayo yalifanyika katika ukumbi wa sherehe wa shule ya Nganza.
Mike alipoondoka Nganza, nyuma yake aliacha gumzo kwa jinsi alivyojichukulia pointi nyingi baada ya kuongea Kiingereza kama mtu aliyezaliwa Uingereza! Aliwavuta wasichana wengi sana.
Miongoni mwa wasichana waliochanganyikiwa juu yake, alikuwa ni Beatrice Rugakingira. Huyu alikuwa ni msichana mrembo kutoka mkoa wa Kagera, aliyekuwa mwanafunzi wa kidato cha pili shuleni hapo.
Beatrice alipomwona Mike akiongea, alijihisi kuchanganyikiwa! Ni wazi nyota ya Mike iliishinda ya Beatrice na kuiburuza vibaya mno. Beatrice alitamani sana kuongea na Mike lakini alishindwa aanze vipi kwa kuwa wasichana wengi walimfuata baada ya malumbano hayo na kumwomba anwani yake na vitu vingine.
Hivyo Beatrice hakubahatika kabisa kuongea naye kitu chochote mpaka anaondoka, jambo hilo lilimuuma sana moyoni mwake lakini yote alimwachia Mungu. Aliamua kuwa mvumilivu akikumbuka methali isemayo milima haikutani lakini binadamu hukutana. Aliamini siku moja angekutana na Mike na kumweleza kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.
Tabia za wasichana katika shule ya Nganza ziligawanyika katika makundi matatu. Walikuwepo waliokuwa na uhusiano wa kimapenzi na wavulana kutoka shule mbalimbali za sekondari mjini Mwanza kama vile Bwiru na Nsumba.
Kundi jingine lilikuwa ni la waliokuwa na uhusiano na wafanyabiashara maarufu mjini humo na kundi la tatu na la mwisho, lilikuwa ni la wasichana walioliwazana wenyewe kwa wenyewe. Hawa waliitwa wasagaji au lusibo.
Tofauti sana na wasichana wengi, Beatrice alikuwa msichana mpole ambaye katika umri wake wa miaka kumi na mitano, kama ilivyokuwa kwa Mike, hakujihusisha na kundi lolote kati ya hayo matatu. Kifupi alikuwa hajawahi kukutana kimwili na mwanamume yeyote, jambo ambalo halikuwa rahisi kwa wasichana wa shule ya Nganza wa wakati ule.
Je nini kitaendelea?  fuatilia RNGM blog

No comments