Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA UHAI WANGU - 6

SIKU ZA UHAI WANGU - 6 Mvulana mwenye akili na pia mcheza muziki, Mike Martin amekutana na msichana mzuri, mwenye mvuto na upole wa hali...

SIKU ZA UHAI WANGU - 6


Mvulana mwenye akili na pia mcheza muziki, Mike Martin amekutana na msichana mzuri, mwenye mvuto na upole wa hali ya juu, Beatrice Rugakingira.
Wawili hao, huku wakiwa hawajawahi hata kukutana kimwili katika maisha yao, wanajikuta wakiangukia katika penzi zito na mahusiano kuanza rasmi huku ahadi ya kutokufanya mapenzi mpaka kuoana ikiwekwa.
Wanakubaliana, baada ya kipindi fulani, Mike anapata nafasi ya kwenda kusomea Shahada ya Uchumi katika Chuo cha Oxford nchini Uingereza. Akiwa njiani, anapata tatizo la kuumwa tumbo ambalo linamfanya kuhitaji kuongezewa damu.
Ndege inashushwa katika Jiji la Copenhagen nchini Denmark. Anapelekwa hospitali, wanapokuja wanafunzi kutoka nchini Tanzania kumuongezea damu, hakuna mwenye kundi kama lake zaidi ya msichana aliyesafiri naye, Laila.
Kinachofanyika, msichana Laila, kwa upendo wake wa dhati, anamuongezea damu Mike na kisa safari kuendelea.

SONGA NAYO...


Baada ya kuandika barua ile, huku machozi yakimtoka, Mike alianza kuisoma, hata yeye mwenyewe alisikia uchungu mwingi moyoni mwake lakini hakuwa na la kufanya. Mpaka wakati ule Mike alikuwa hajaamini kabisa kama yaliyokuwa yakitokea katika maisha yake yalikuwa kweli au ilikuwa ni ndoto na muda si mrefu angezinduka kutoka usingizini.
Kwa upande mwingine, Mike alijichukia mwenyewe na hakuona sababu ya kuendelea kuishi lakini vilevile hakuona sababu ya kujiua. Hivyo akaamua kumwachia Mungu afanye kazi yake, atakavyo mwenyewe.
Kilichomsumbua akilini mwake baada ya kuiandika barua ile ni kwa njia gani angemkabidhi Beatrice! Kwa jinsi alivyomfahamu Beatrice alijua barua ile ingemchanganya sana na si ajabu asingeyaamini majibu.
Kama msichana ni lazima angehisi ile ilikuwa njama ya kuachwa kijanja. Ili kumhakikishia kuwa aliyoaandika yalikuwa na ukweli, Mike aliamua kuzichukua karatasi za majibu ya Bugando na Medical Research na kuziambatanisha pamoja na barua ile na kuandika.
Tanbihi: Nyuma ya hii barua nimeambatisha karatasi zote za majibu ili upate kuamini.
Baada ya kuisoma barua ile Mike alijitupa kitandani bila kuvaa nguo, hakupata hata lepe la usingizi. Kulipokucha alinyanyuka kitandani kizembe na kuingia bafuni kuoga, baada ya kuoga alichukua nguo safi na kuvaa.
Akiwa tayari kwenda kazini kwake, kwa muda alijisikia kusahau kidogo habari ya majibu lakini ghafla taswira ilimrejea tena na pale pale akaishiwa nguvu za miguu na kukaa kitini. Hakujisikia tena kufanya kazi
Alichokifanya baada ya hapo ni kunyanyua simu na kupiga kiwandani Mwatex.
"Hallow nani anaongea?" Aliuliza simu ilipopokewa.
"Monica!" Katibu Muhtasi wake akajibu.
"Tafadhali waeleze kuwa hali yangu si nzuri sitafika kazini, sawa?"
"Unaumwa nini bosi?" Aliuliza Monica, ambaye naye siku zote juhudi zake za kumwinda Mike hazikukoma.
"Nimekwambia sijisikii vizuri inatosha, unataka kujua nini zaidi?” Aliuliza Mike kwa sauti ya ukali.
"Samahani bosi," alitamka Monica kwa upole.
Baada ya kukata simu aliyopiga ofisini, palepale Mike alizungusha namba ya Beatrice.
"Beatrice!"
"Naam darling," aliitika
"Nina maongezi na wewe na ningependa maongezi hayo tuyafanye sehemu ya faragha kidogo sijui unapendelea sehemu gani?"
"Ni kuhusu mipango yetu ya harusi?"
"Hapana mpenzi wangu."
"Ni juu ya nini tena Mike mbona unanirusha roho?"
"Ah! Ni mambo ya kawaida tu kati yangu mimi na wewe."
"Sawa tukutane Salma Cone basi!"
Salma Cone ni sehemu maarufu sana ya kuuza vinywaji na barafu mjini Mwanza.
"Hapana Beatrice, sehemu hiyo si nzuri sana kwa jambo linalotaka kuliongea, labda nikupitie hapo halafu twende sehemu nyingine."
"Wapi sasa?"
"Twende kisiwa cha Saa Nane!"


Kilikuwa ni kisiwa kilichokuwa kilometa moja kutoka mjini Mwanza, na ili ufike huko ilikuwa ni lazima upande boti. Wakazi wa Mwanza walipendelea kutembea huko siku za mwisho wa wiki.
"Sawa basi nipitie Salma Cone nitakuwa nakusubiri hapo, sijui ni saa ngapi?'
"Saa kumi jioni!"
Mpaka wakati huo Mike alikuwa akifikiria hali ingekuwaje mara tu Beatrice atakapoisoma ile barua, alijua angeumia mno kwa muda alioupoteza na aibu ambayo angeipata. Ni wazi angekosa mahali pa kuficha uso wake.
Mike aliligundua suala hilo lakini hakuwa na la kufanya, ilikuwa ni lazima aseme ukweli. Ndiyo alimpenda sana Beatrice lakini asingeweza kumwoa na kumwambukiza UKIMWI afe! Bado Mike alimshukuru Mungu kwa kuepusha tendo la ndoa kati yao.
***
Saa kumi kasoro dakika kumi Mike aliliegesha gari lake mbele ya jengo la Salma Cone mtaa wa Bantu. Aliamua kuwahi mapema ili walau awe anakunywa juisi wakati akimsubiri Beatrice.
Aliteremka haraka na kuingia ndani ya mgahawa wa Salma Cone. Alishangaa kumkuta Beatrice amekwishafika na tabasamu likiwa limemjaa usoni.
"Karibu Mike," Beatrice alinyanyuka kitini na kumkumbatia Mike akampiga mabusu matatu usoni! Watu wote waliokuwa ndani ya mgahawa walishangaa.


"Asante darling, nilifikiri nimewahi kumbe nimechelewa."
"Hapana, hujachelewa kwani hata mimi nimefika kama dakika kumi tu zilizopita. Nimewahi kwa sababu nina hamu kubwa ya kukijua hicho unachotaka kunieleza."
Mike alinyanyua uso wake na kumwangalia Beatrice.
"Mike mbona macho yako mekundu, unaumwa au?" Beatrice alihoji.
Palepale Mike alianza kulia tena.
"Ni mambo makubwa sana Beatrice na sijui kama utanielewa."
"Mambo gani hayo?"
"Twende Beatrice!" Mike alinyanyuka kitini huku akijifuta machozi!
Baada ya wote kuketi katika viti vyao Mike aliliondoa gari hadi karibu na Hoteli ya Tilapia kulikokuwa na kivuko cha kwenda kisiwa cha Saa Nane. Aliliegesha gari na wote wakateremka bila kuchelewa. Walikata tiketi na kupanda boti ndogo iliyowapeleka moja kwa moja hadi kisiwani. Kwa kuwa siku hiyo haikuwa mwisho wa wiki, walijikuta wakiwa wawili tu kisiwa kizima.
Mike na Beatrice walitembea mkono kwa mkono huku wakipita wanyama kama simba na chui katika seng'enge zao bila kuwajali. Lengo lao siku hiyo halikuwa kuwaangalia wanyama.
Walipandisha moja kwa moja hadi kilimani kwenye mapango yaliyo juu. Mtu akiwa huko maji ya Ziwa Viktoria huonekana kwa chini kabisa kama uko kwenye nyumba ya ghorofa tano. Beatrice aliangalia chini akasikia kizunguzungu.


"Mike hapa mtu akidondoka si anakufa kabisa?"
"Inawezekana maana maji yapo mbali sana."
"Lakini Mike, hebu tuyaache hayo bwana, nieleze kitu ulichoniitia."
Mike alinyamaza kwa muda na baadaye, huku akitetemeka alimkabidhi Beatrice barua! Beatrice aliipokea barua ambayo juu ya bahasha iliandikwa jina lake. Kabla hajaifungua alimwangalia Mike na kucheka.
"Na wewe huwa unapenda sana kunifanyia surprise."
Beatrice aliifungua barua ile na kuanza kuisoma, na kadri alivyozidi kuisoma ndivyo jasho jingi lilivyozidi kumtoka mpaka nguo alizovaa zikalowa kabisa. Alipomaliza kuisoma upande mmoja akageuza upande wa pili na kuanza kuzingalia zile karatasi zenye majibu.
"Mike, yaani umekaa chini ukaona huu ndio ujanja wa kuniacha, siyo? Mike! Mike! Mike! Mike! Mwogope Mungu Mike! Kumbuka muda ulionipotezea Mike, nimeacha wachumba wangapi kwa sababu yako? Mike leo uniache kinyama kiasi hiki? Eti kwa sababu tu umekutana na wasichana wazuri zaidi yangu! Haiwezekani.
Lakini kwa nini unanifanyia ukatili huu? Mike nimekukosea nini Mike? Ni heri nife kuliko kuiona aibu hii."
Alipomaliza tu kusema maneno hayo palepale Beatrice alijirusha kutoka juu kwenye pango walikokuwa wamekaa na kuanza kuporomoka kuelekea majini!


"Beatriceeee what have you done?" (Beatrice umefanya nini?) Mike alipiga kelele alipomwona Beatrice akielekea majini.
Eneo ambalo Beatrice alitumbukia ni eneo lililokuwa na kibao kilichoonya watu wasiogelee katika eneo hilo kwa kuwa kulikuwa na mamba wala watu.
Mike alipokiona kibao kile alichanganyikiwa akajua lazima Beatrice ataliwa na mamba. Alianza kuteremka mlima akikimbia kuelekea majini. Aliogopa sana mamba lakini alikuwa ameamua kuutoa uhai wake kwa ajili ya Beatrice kwani hata kama asingejikatisha hakuwa na maisha tena mbele!
Kabla hajaingia ndani ya maji aliona damu nyingi imetapakaa juu ya maji, akashtuka na kuamini kwamba Beatrice alikuwa tayari amekwishaliwa na mamba! Aliamini hivyo kwa kuwa kila alipotupa macho hakuweza kumwona Beatrice.
Je nini kitaendelea?
Je Beatrice amekufa?

No comments