Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA UHAI WANGU -3

SIKU ZA UHAI WANGU 3 Mvulana aliyekuwa na uwezo mkubwa darasani ambaye alikuwa akisoma katika Shule ya Wavulana ya Nsumba ya jijini Mwanz...

SIKU ZA UHAI WANGU 3
Mvulana aliyekuwa na uwezo mkubwa darasani ambaye alikuwa akisoma katika Shule ya Wavulana ya Nsumba ya jijini Mwanza, Mike Martin anajikuta akiwavutia wasichana wengi hasa wa Shule ya Wasichana ya Ngaza.
Anajikuta akipokea barua nyingi kutoka kwa wasichana hao lakini kitu cha ajabu, hakutaka kuwa na msichana yeyote yule. Mbali na uwezo wake mkubwa darasani, Mike alikuwa na uwezo mkubwa wa kucheza muziki kitu kilichowafanya wanafunzi kumuita jina la Double Mhuku wakimfananisha na mwanamuziki Michael Jackson.
Upande wa pili, msichana mpole na mtaratibu ambaye naye hakuwahi kukutana na mwanaume kimwili, ambaye alikuwa akisoma katika SHule ya Wasichana ya Ngaza anajikuta kuvutiwa na MIke, moyo wake unaweweseka, mapnzi mazito yanaugubika moyo wake.
Anaogopa kwa kuwa hajawahi kuzungumzia mapenzi na mvulana yeyote yule. Anapoona ameshindwa kabisa kuongea na Mike, anajukuta akijifariji kwa kusema kwamba milima haikutani ila binadamu hukutana, ipo siku atakutana tena na Mike.
SONGA NAYO...
Urafiki wao uliendelea mpaka Mike akamaliza kidato cha nne na kujiunga na kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Nyakato iliyoko Bukoba ambako alisoma hadi kumaliza kidato cha sita.
Baada ya kumaliza kidato cha nne Beatrice hakuendelea na kidato cha tano bali alijiunga na Chuo cha Uuguzi cha Rubya ambacho pia kipo mkoani Kagera, kwa kozi ya miaka minne ya Uuguzi na Ukunga.
Baada ya kumaliza kidato cha sita, Mike alibahatika kupata nafasi ya kwenda kusomea Shahada ya Uchumi katika Chuo Kikuu cha Oxford, nchini Uingereza. Kabla hajaondoka, walikuwa tayari wamepanga kuoana baada ya kumaliza masomo yao. Mike alimsihi Beatrice awe mvumilivu na mwaminifu katika kipindi chote ambacho angekaa Uingereza ili atakaporudi wafunge ndoa yao!
***
Mike alisafiri hadi Dar es Salaam ambako alipokewa na baba yake mdogo, mzee Joshua, ambaye alimfanyia taratibu zote za usafiri.
Kabla ya safari yake ya Uingereza yeye na mtoto wa mzee Joshua, Consolatha, walikwenda Zanzibar ambapo Mike alinunua nguo na vitu mbalimbali vya safari.
Wakiwa njiani kutoka Zanzibar waliongea mambo mengi kuhusu maisha. Mike alimuuliza Consolatha alichotaka kufanya katika maisha yake. Consolatha alimjibu kuwa kama angefanikiwa kumaliza na kufanya vizuri kidato cha sita wazazi wake walikuwa wamepanga aende Marekani kwa mama yake mdogo ambako angesomea Udaktari wa Mifupa.
Alidai hiyo ilikuwa ndiyo kazi pekee ambayo angependa kuifanya maishani mwake. Siku mbili baadaye, Mike alipanda ndege ya Shirika la Ndege la Uingereza, British Airways, kuelekea Uingereza kupitia Copenhagen. Alikuwa ni mtu mwenye furaha kupita kiasi, aliona ndoto zake zikitimia! Katika maisha yake alitaka kuwa mtu mkubwa na mwenye madaraka katika nchi na kwa kwenda kusoma Uingereza aliamini hilo lilikuwa limetimia.
***
Alikuwa wa kwanza kukaa kwenye kiti cha watu wawili alichokuwa amepangiwa. Baadaye alikuja msichana mmoja wa Kisomali na kukaa jirani yake. Msichana huyo ama kwa maringo au kwa kujiona mzuri, hakumsalimu Mike na alionekana mwenye dharau nyingi! Jambo hilo lilimkera sana Mike naye akaamua kukaa kimya pia.
Baada ya kukaa kitini msichana yule alichukua gazeti la Ebony la mwezi huo akijifanya kutogundua kuwa kuliwa na mtu pembeni yake.
Mike naye hakutaka kujirahisi. Alichukua gazeti lake la Uwazi na kuanza kusoma taratibu. Hakuna aliyemjali mwenzake. Muda mfupi baadaye ndege iliruka na dakika arobaini na tano baadaye ilitua katika Uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta, Nairobi, nchini Kenya bila Mike wala msichana yule kusemeshana.
Lakini kabla ndege haijaruka kutoka Nairobi kuendelea na safari, msichana yule alizinduka rasmi na kuanza maongezi.
“Hi, I am Laila, and you?” (Hujambo, mimi naitwa Laila, wewe ni nani?).
“My name is Mike. Hi Leila!” (Ninaitwa Mike. Hujambo Laila!).
“Fine thank you. What’s your destination sir?”
(Sijambo! Safari yako inaishia wapi, bwana?).
“My destination is UK, what about you?”
(Safari yangu inaishia Uingereza, wewe je?).
“I’m tavelling to Capenhagen. I’m a student at the University of Copenhagen taking Medicine and Public Health. What are you doing in the UK?” (Mimi nakwenda Copenhagen ambako nasoma Udaktari na Afya ya Jamii. Je, wewe unafanya nini Uingereza?).
“I’m going to join the Univesity of Oxford for my Bachelor Degree in Economics and Extra Education in Computer Science” (Ninakwenda Chuo Kikuu cha Oxford kusomea Shahada ya Kwanza ya Uchumi na Elimu ya Kompyuta).
“Oxford?” Laila aliuliza kwa mshangao.
“Yes?” (Ndiyo).
“It’s the most expensive university in the United Kingdom! Only very bright or rich students do join there! How did you get the chance? You must either be very bright or rich! (Ni chuo cha gharama kubwa sana Uingereza na wanafunzi wenye akili nyingi ndio hujiunga, wewe ulipataje nafasi hiyo? Wewe ni tajiri au una akili nyigi mno!).
“I’m neither rich nor bright, it was just a game of luck”. (Mimi sio tajiri na wala sina akili nyingi mno lakini ilikuwa ni bahati tu).
Mazungumzo hayo mafupi yaliwaunganisha Mike na Laila katika hali ya urafiki. Tangu dakika hiyo maongezi yalipamba moto wakawa kama watu waliofahamiana miaka kumi kabla!
Saa tano baadaye, wakiwa bado angani lakini wakiwa wamekaribia kabisa kutua katika Uwanja wa ndege wa Copenhagen uliokuwa mwisho wa safari ya Laila, bahati mbaya ilimkumba Mike.
Alianza kujisikia kichefuchefu na tumbo likaanza kumkata na mtu wa karibu kwake kwa wakati ule hakuwa mwingine bali Laila. Alimweleza tatizo lake akitaka amsaidie. Laila alitoa chupa ya dawa ya maji iliyoandikiwa Mucaine Suspension na kumpa Mike akanywa lakini bado haikumsaidia.
Hali ilizidi kuwa mbaya kadri dakika zilivyozidi kwenda. Mike akaanza kutapika, ikabidi Laila awataarifu wahudumu ndani ya ndege juu ya tatizo hilo ambapo walimfanyia huduma ya kwanza bila mafanikio.
Ndege ilipotua Copenhagen ilibidi safari ya Mike ikatishwe na akimbizwe haraka sana hospitali ambako iligundulika kwamba alikuwa na tatizo la kujisokota kwa utumbo. Ugonjwa huo ulitamkwa na madaktari kama Intestinal Obstruction.
Hali ya Mike ilikuwa mbaya mno na ili kuokoa maisha yake ilibidi mipango ifanyike haraka iwezekanavyo ili afanyiwe upasuaji kurekebisha hali ya kujisokota kwa utumbo. Hata hivyo, kabla ya kufanyiwa operesheni hiyo zilihitajika chupa tatu za damu.
Laila, ambaye wakati wote alikuwepo kumsaidia Mike ambaye hakuwa na mtu aliyemfahamu zaidi yake nchini Dernmark, ilibidi aende chuoni kwake ambako aliwataarifu wanafunzi kumi wa Kitanzania waliokuwa wakisoma katika Chuo cha Kikuu cha Copenhagen. Aliwataka waongozane naye hadi hospitali kujitolea damu ili kuyaokoa maisha ya Mtanzania mwenzao.
Kuna makundi manne ya damu ambayo binadamu anaweza kuwa nayo, ambayo ni ama kundi A, B, AB na O. Kinachofanya makundi ya damu yatofautiane ni Protini ziitwazo Agglutinogen. Mtu mwenye kundi “A” damu yake huwa na protini Agglutionogen na mtu mwenye kundi “B” damu yake huwa na Agglutionogen.
Mwenye kundi “O” huwa hana aina yoyote ya Agglutionogen. Hata hivyo, ndani ya damu ya mwanadamu kuna maaskari au “antibody” kwa Kiingereza ambao hupambana na hizi Agglutionogens, maaskari hawa huitwa Agglutins.
Mtu mwenye kundi “A” la damu huwa na maaskari waitwao Agglutinions Anti B na mwenye kundi “B” huwa na Agglutinis Anti A na mwenye kundi “AB” huwa hana aina yoyote ya maaskari hao. Kwa sababu hii mtu mwenye kundi “AB” anaweza kupokea damu kutoka kwa kundi lolote la damu!
Kwa sababu mtu mwenye kundi “O” la damu ana maaskari wote wa “A” na “B” hupokea damu kutoka kwa mtu mwenye kundi “O” peke yake. Hivyo, Mike alihitaji damu kutoka kwa mtu mwenye kundi “O” peke yake.
Wanafunzi wote kumi walipopimwa damu zao hazikushabihiana na damu ya Mike, wengi walikuwa kundi “A” na “B”. Alipoona hivyo, Laila aliomba ajaribu kupimwa yeye. Kwa bahati nzuri alipopimwa damu yake ilikuwa “O” na kushabihiana na damu ya Mike. Palepale Laila alitolewa damu chupa tatu ili kuokoa maisha ya mtu waliyekutana naye kwenye ndege! Wanafunzi wa Tanzania walimshukuru sana Laila kwa moyo wa ukarimu aliouonyesha.
Wiki moja baada ya kufanyiwa operesheni, Mike alikuwa mzima kabisa. Alitoa shukurani za pekee kwa Laila na wanafunzi wengine wa Kitanzania waliomsaidia katika matatizo yake. Akaendelea na safari yake moja kwa moja hadi Uingereza ambako aliendelea na masomo kama kawaida.
Je nini kitaendelea?
Je Mike huu ndiyo mwisho wa Mike na msichana Laila?

No comments