Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA UHAI WANGU -4

SIKU ZA UHAI WANGU -4 Mvulana mwenye akili na pia mcheza muziki, Mike Martin amekutana na msichana mzuri, mwenye mvuto na upole wa hali y...


SIKU ZA UHAI WANGU -4

Mvulana mwenye akili na pia mcheza muziki, Mike Martin amekutana na msichana mzuri, mwenye mvuto na upole wa hali ya juu, Beatrice Rugakingira.
Wawili hao, huku wakiwa hawajawahi hata kukutana kimwili katika maisha yao, wanajikuta wakiangukia katika penzi zito na mahusiano kuanza rasmi huku ahadi ya kutokufanya mapenzi mpaka kuoana ikiwekwa.
Wanakubaliana, baada ya kipindi fulani, Mike anapata nafasi ya kwenda kusomea Shahada ya Uchumi katika Chuo cha Oxford nchini Uingereza. Akiwa njiani, anapata tatizo la kuumwa tumbo ambalo linamfanya kuhitaji kuongezewa damu.
Ndege inashushwa katika Jiji la Copenhagen nchini Denmark. Anapelekwa hospitali, wanapokuja wanafunzi kutoka nchini Tanzania kumuongezea damu, hakuna mwenye kundi kama lake zaidi ya msichana aliyesafiri naye, Laila.
Kinachofanyika, msichana Laila, kwa upendo wake wa dhati, anamuongezea damu Mike na kisa safari kuendelea.
SONGA NAYO...
Miaka miwili baada ya Mike kufika nchini Uingereza, kulitokea ugonjwa wa ajabu uliopunguza kinga ya mwili kupambana na magonjwa ambao Marekani na nchi nyingi za Ulaya uliitwa Acquired Immuno Deficiency Syndrome au AIDS na Tanzania uliitwa Upungufu wa Kinga Mwilini au UKIMWI. Ugonjwa huo ulitangazwa kuwa ni ugonjwa hatari duniani kote baada ya kugundulika kuwepo wagonjwa kadhaa nchini Marekani na Uganda, Afrika Mashariki.
Njia za kuambukiza ugonjwa huo zilipotajwa zilikuwa ni pamoja na ile ya kuongezewa damu. Mike aliposikia hivyo, alishtuka lakini alijipa moyo na kuamini Laila asingekuwa nao kwa jinsi afya yake ilivyokuwa nzuri.
“Hakuonekana kuwa mtu mwenye dalili za ugonjwa huu,” alisema baada ya kuzisoma dalili zake.
Miaka sita baadaye Mike alimaliza masomo yake. Yalikuwa ni masomo ya miaka mitano lakini aliongeza mwaka mmoja ambao aliutumia kusomea Uongozi wa Elimu ya Kompyuta, lengo lake likiwa kupata kazi nzuri baada ya kurudi Tanzania.
Akiwa njiani kurudi Tanzania, Mike aliamua kupita Copenhagen kumshukuru Laila, mtu aliyeokoa maisha yake! Alimnunulia zawadi nzuri ya friji kama ishara ya shukurani zake. Alipofika Copenhagen alishangazwa na taarifa alizosikia kuwa Laila hakuwepo chuoni, alirudishwa Mogadishu baada ya kuugua kifua kikuu kwa muda mrefu na hali yake kudhoofika.
Mike alitamani sana kumwona Laila lakini hakuwa na uwezo wa kusafiri hadi Mogadishu. Badala yake alipanda ndege moja kwa moja hadi Nairobi na kuunganisha kwa ndege nyingine hadi Dar es Salaam.
Uwanjani Dar es Salaam alipokewa na mzee Joshua, mkewe na Lydia, mdogo wake Consolatha. Hakushangaa kwa nini Consolatha hakuwa pale. Alijua ni lazima kwa wakati huo alikuwa amefanya vizuri katika masomo yake ya kutimiza ndoto yake ya kwenda Marekani kusomea Udaktari wa Mifupa.
Wakiwa ndani ya gari kuelekea nyumbani kwa mzee Joshua, Mike alishindwa kuvumilia. Akajikuta akiuliza kama Consolatha alifanikiwa kutimiza ndoto yake. Cha kushangaza ni kwamba hakuna mtu aliyelijibu swali lake ingawa alikuwa na uhakika kabisa kuwa watu wote walimsikia.
Walipofika nyumbani alikaribishwa ndani na yakafanyika maombi maalum kumshukuru Mungu kwa kumrudisha Mike salama nyumbani Tanzania.
Baada ya maombi hayo kabla ya chakula cha jioni Mike alianza kuwasimulia yote yaliyojitokeza akiwa Uingereza, likiwemo tatizo lake la kuugua njiani na kufanyiwa upasuaji nchini Denmark.
“Namshukuru sana yule dada wa Kisomali vinginevyo nisingekuwa hai maa…” Mike alishtuka ghafla, dakika mbili baadaye alianza kulia.
“Mike mbona unalia tena?” Mzee Joshua alimuuliza.
“Yaani kumbe Consolatha alishafariki na hamjanieleza?” Mike alisema huku ameikodolea macho picha kubwa iliyokuwa imetundikwa ukutani ikiwa imezungukwa na maandishi, 'Tulikupenda mwanetu lakini Mungu alikupenda zaidi, Mungu ailaze roho yako mahali pema peponi.'
“Tulikuwa tunasubiri upumzike ili tukueleze maana tulishindwa kukutaarifu ukiwa Uingereza tukiamini tungekuvurugia masomo yako maana ulimpenda sana marehemu dada yako,” alisema mzee Joshua.
“Haya nielezeni basi,” Mike alisema huku akijifuta machozi.
“Dada yako alimaliza shule na kufanya vizuri sababu alipata daraja la kwanza kidato cha sita alipata pointi nne. Mama yake mdogo aliyekuwa Marekani, kama zawadi kwa alivyofanya vizuri katika wanafunzi wote Tanzania, alimwita akasomee Udaktari wa Mifupa, kazi ambayo marehemu aliipenda.
Kama ulivyofanya wewe, Consolatha naye aliamua kwenda Zanzibar kununua nguo za kusafiri nazo, akiwa njiani kutoka Zanzibar boti aliyokuwa akisafiri nayo ilizama, watu wote waliokuwa ndani ya boti hiyo hawakuonekana na hata boti yenyewe mpaka leo hii bado iko majini! Hivyo, Consolatha alifariki na hatukufanikiwa hata kuupata mwili wake.”
“Eee Mungu wangu ilaze roho ya Consolatha mahali pema peponi,” Mike alisema huku machozi yakimtoka na kunyanyuka kwenda kuibusu picha ya Consolatha.
***
Wakati wote Mike akiwa nje ya nchi, Beatrice alijitahidi kuwa msichana mwaminifu. Hakutaka kabisa kuvunja ahadi waliyowekeana na hakutaka kuharibu ubikira wake. Aliamini kwamba hiyo ndiyo zawadi pekee ya kumtunzia Mike mpaka siku ya ndoa yao.
Alipomaliza masomo yake ya Uuguzi na Ukunga, Beatrice aliajiriwa na Hospitali ya Mkoa wa Kagera kama Muuguzi Mkunga, na mawasiliano yake na Mike yalikuwa mazuri. Mike alimpigia simu moja kwa moja kutoka Uingereza karibu kila mwezi na kumtumia zawadi nyingi mara kwa mara.
Beatrice alisumbuliwa na wanaume wengi wakitaka kumwoa! Aliwakataa wachumba wasiopungua watatu akiwemo Meneja wa Kiwanda cha Sukari cha Bukoba kwa sababu ya Mike.
Tarehe 12 Septemba, 1986, saa 10 jioni, ikiwa ni miaka sita baada ya Mike kuondoka nchini, Beatrice akiwa amejipumzisha chumbani mwake, simu iliita ghafla naye aliipokea. Ilikuwa ni simu ya Mike.
“Hi! Darling habari za Uingereza?”
“Sio Uingereza mama, hapa nipo Bongo.”
“Dar? Mbona ghafla hivyo na hujaniambia?”
“Nilitaka kukufanyia surprise! (kukushtukiza) kwa hiyo, kesho naingia Mwanza, nakuomba uje Mwanza tukutane sawa?”
“Nitakuwepo,” Beatrice alijibu na kuongeza: “Jamani Mike miaka mingi sijakuona mpenzi wangu, nafikiri umezidi kuwa mzuri eh!” Beatrice alimwaga sifa.
“Darling utaniona kesho kutwa, lakini nafikiri nimekuwa mbaya zaidi” Mike alitania.
“Kama umekuwa mbaya basi mimi sikutaki tena,” Beatrice aliongeza utani.
“Acha utani wewe, tafadhali njoo tuongee mipango yetu ya ndoa wakati umefika sasa.”
***
Kwa kawaida, meli kutoka Bukoba huwasili Mwanza saa 12:30 asubuhi lakini Septemba 14, 1986 saa 11:00 alfajiri Mike alikuwa tayari amekwishaamka. Alikuwa na hamu kubwa ya kumwona Beatrice baada ya miaka karibu saba bila kumtia machoni.
Baada ya kufanya mazoezi na kuoga aliamua kupumzika na kungoja muda utimie ili aende bandarini kumpokea mchumba wake Beatrice, mwanamke aliyempenda kuliko wanawake wote chini ya jua. Mwanamke ambaye ndiye angekuwa wa kwanza kuvunja naye amri ya sita.
Saa 12:00 asubuhi Mike alikuwa ndani ya teksi aliyoikodi toka nyumbani kwao, Nyakato-Mecco, akielekea bandarini kumpokea kipenzi chake, Beatrice.
Dakika 15 baadaye teksi aliyokodi Mike iliegesha nje ya lango la bandari ya Mwanza na kwa mbali Mike aliweza kuiona meli ya MV Viktoria ikiwasili.
Meli ilipotia nanga moyo wake ulianza kudunda, utafikiri moyo wa mtu aliyekuwa akisubiri kuingia kwenye usaili wa kazi. Alikuwa na hamu kubwa ya kumwona Beatrice na moyoni alihisi furaha ya ajabu.
Alishindwa kuelewa ingekuwa furaha ya aina gani pindi angemtia Beatrice kwenye mboni ya macho yake. Abiria walianza kuteremka mmoja baada ya mwingine. Hata hivyo, Beatrice hakuonekana!
‘Labda aliahirisha safari nini?’ Mike alijikuta akijisemea kwa mshangao.
Akiwa karibu akate tamaa, ghafla alimwona Beatrice akiteremka ngazi taratibu ambapo bila kupoteza muda na bila aibu, alikimbia mbio kuelekea kwenye ngazi akikatiza katikati ya watu mpaka akamfikia. Beatrice alipomwona alimrukia na kumkumbatia.
“Ooh darling! Is it you?” (Mpenzi ni wewe kweli?) Beatrice aliuliza.
“It’s me Beatrice.” (Ni mimi) Mike alijibu kwa sauti ya juu.
“I can’t believe my eyes.” (Siyaamini macho yangu) Beatrice alisema huku machozi ya furaha yakimtoka.
Waliangushana chini huku wakiwa wamekumbatiana na watu wote waliokuwa pale walishangaa. Dakika tano baadaye wote walikuwa wima wakiwa wamekumbatiana, wakilia kwa furaha! Kila mmoja alimwona mwenzake kuwa amezidi uzuri.
“Hawa kweli wanapendana!” akinamama waliokuwa jirani walisikika wakisema.
Baadaye Mike alichukua begi la Beatrice na wote wakaingia ndani ya gari na kuondoka.
“Dereva, moja kwa moja hadi Natta Hotel, sawa?” Mike aliamuru.
“Hakuna taabu!” dereva alijibu na kuliondoa gari kuelekea alikoelekezwa.
Baada ya kusema hayo, Mike alimgeukia Beatrice ambaye alikuwa bado akilia kwa furaha.
“Za siku mpenzi?”
“Niache kwanza nipumzike Mike, nina mengi ya kuongea na wewe kwa sasa kifua kimenibana, nikitulia nitakusimulia mengi lakini nashukuru Mungu amekurudisha salama mpenzi wangu.”
Dakika tano baadaye gari liliegeshwa nje ya Hoteli ya Natta, Mike akamlipa dereva pesa zake, akachukua begi na kumshika Beatrice mkono. Walikaa hotelini ambako Mike alipanga chumba. Baada ya kuweka mizigo vizuri walijitupa kitandani.
“Nafikiri sasa umetulia hebu nieleze,” Mike aliyaanzisha maongezi.
“Ni mengi lakini kifupi nilikukumbuka sana, vilevile bado ninakupenda, sitaacha kukupenda milele Mike.”
Majira ya saa kumi jioni, Mike alirudi nyumbani kwao kuongea na wazazi wake. Akawaomba wamruhusu aende mjini kwa shida zake na kuwafahamisha kwamba asingerudi mpaka asubuhi siku iliyofuata.
Alidanganya kuwa kulikuwa na sherehe iliyoandaliwa na rafiki zake kumpongeza. Alilazimika kusema hivyo kwa sababu wazazi wake walikuwa bado hawajamfahamu Beatrice.
Alichukua begi lililokuwa na zawadi alizomnunulia Beatrice na kuondoka nalo.
Alipofika hotelini alimkuta Beatrice akiwa bafuni anaoga, hakupoteza muda, naye akavua nguo zake, akachukua taulo na kuingia bafuni ambako walioga pamoja.
Ilikuwa ni mara ya kwanza kwao kuoga pamoja tangu wafahamiane. Wakati wakioga ghafla Beatrice alianza kujisikia msisimko wa ajabu mwilini, ilikuwa ni mara yake ya kwanza kumwona mwanaume akiwa kama alivyozaliwa.
“Mike!”
“Naam, darling.”
“NImevumilia kwa muda mrefu sana, mwenzio nimeshindwa, tafadhali naomba…naomba tu…tu..” baada ya kusema hayo alimkumbatia Mike kwa nguvu.
“Beatriceeeee!” Mike alisema kwa ukali.
“Be…e! Mike!” Beatrice aliitikia.
“Kumbuka ahadi yetu na utulie mpenzi,” Mike alisisitiza.
Ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Beatrice kumsikia Mike akiongea kwa sauti ya ukali kiasi kile. Alitambua kuwa alikuwa amemkasirisha, hakupoteza muda, aliamua kumwomba msamaha na Mike alimsamehe.
Je nini kitaendelea?
Je Mike ataendelea kuwa mvumilivu mpaka ndoa?
Je wawili hawa wataoana?

No comments