Page Nav

HIDE

Breaking News:

latest

SIKU ZA UHAI WANGU - 5

SIKU ZA UHAI WANGU - 5 Mvulana mwenye akili na pia mcheza muziki, Mike Martin amekutana na msichana mzuri, mwenye mvuto na upole wa hali ya...

SIKU ZA UHAI WANGU - 5
Mvulana mwenye akili na pia mcheza muziki, Mike Martin amekutana na msichana mzuri, mwenye mvuto na upole wa hali ya juu, Beatrice Rugakingira.
Wawili hao, huku wakiwa hawajawahi hata kukutana kimwili katika maisha yao, wanajikuta wakiangukia katika penzi zito na mahusiano kuanza rasmi huku ahadi ya kutokufanya mapenzi mpaka kuoana ikiwekwa.
Wanakubaliana, baada ya kipindi fulani, Mike anapata nafasi ya kwenda kusomea Shahada ya Uchumi katika Chuo cha Oxford nchini Uingereza. Akiwa njiani, anapata tatizo la kuumwa tumbo ambalo linamfanya kuhitaji kuongezewa damu.
Ndege inashushwa katika Jiji la Copenhagen nchini Denmark. Anapelekwa hospitali, wanapokuja wanafunzi kutoka nchini Tanzania kumuongezea damu, hakuna mwenye kundi kama lake zaidi ya msichana aliyesafiri naye, Laila.
Kinachofanyika, msichana Laila, kwa upendo wake wa dhati, anamuongezea damu Mike na kisa safari kuendelea.
Baada ya kurudi Tanzania na zawadi nyingi, mahusiano yake na mpenzi wake yanazidi kupamba moto, kuna siku Beatrice anatamani kufanya mapenzi na Mike, ila mpenzi wake huyo anakataa kwa kumkumbusha kuhusu ahadi yao kwamba wasingeweza kufanya mapenzi mpaka wafunge ndoa, Beatrice anakuwa mpole.
SONGA NAYO...
Baada ya kuoga walivaa na kutoka kwenda Hoteli ya Continental iliyokuwa maarufu mjini humo kwa kupika chakula kizuri.
Mike alivaa suti nyeusi na Beatrice alivaa suruali ya jeans iliyombana vizuri na tisheti nyeupe iliyoandikwa kifuani “My virginitiy is just for you only” (Bikira yangu ni kwa ajili yako wewe tu).
“Beatrice, ulinunua wapi nguo hii?” Mike alimuuliza.
“Dukani, huko Kampala.”
“Kwa nini ulinunua?”
“Nilitaka kukuonyesha nipo kwa ajili yako Mike.”
Mike alimkumbatia Beatrice na kumbusu kwenye paji la uso.
“Nakupenda Beatrice, nitakupenda milele na leo nakutamkia kuwa nitakuoa ili uwe mke wangu wa milele na milele.”
Beatrice akaanza kulia kwa furaha, hakuyaamini masikio yake kama yalisikia sawa maneno yale.
“Asante Mike, hata mimi nimevumilia vya kutosha nafikiri sasa ni vizuri tukaishi pamoja.”
Baada ya chakula wakarudi tena hotelini na usiku huo walikesha wakiongea kuhusu mipango yao ya ndoa na kila mtu alionekana kuwa na hamu ya harusi kumzidi mwenzake.
Siku iliyofuata baada ya kuweka mambo sawa Beatrice alirudi Bukoba huku tayari wakiwa wamepanga kwamba Mike angekwenda Bukoba kwa wazazi wake kujitambulisha.
***
Mwezi uliofuata Mike aliajiriwa na Kiwanda cha Nguo cha Mwatex kama Meneja Utawala. Kabla ya kuanza kazi alikwenda Dar es Salaam kukomboa bandarini mali zake zote alizozinunua Uingereza. Kulikuwa na malori matano na matela yake, magari madogo mawili, moja la kwake la kutembelea aina ya BMW na jingine la baba yake aina ya Mitsubishi Canter tani tatu na nusu.
Pia alinunua mashine ya kusaga, kuchana mbao, mashine za kuchapisha nakala, kompyuta ishirini na vyombo vya ndani.
Kutokana na mali alizokuwa nazo pamoja na kazi yake ya umeneja akiwa katika umri mdogo, jina lake lilivuma kupita kiasi mjini Mwanza.
Alifahamika karibu na kila mtu hadi watoto wadogo. Alipopita mitaani watoto walimshangilia Mike! Mike! Mike! Kwa muda mfupi tu alikuwa ameshakuwa maarufu kuliko hata Meya wa mji huo.
Gari lake la BMW lilizidisha umaarufu wake maradufu kwani hapakuwa na mtu mwingine mwenye gari kama hilo mjini Mwanza.
Miezi michache baada ya Mike kuanza kazi, alipewa nyumba ya kuishi katika nyumba za wafanyakazi wa Mwatex zilizokuwa mlimani Bugando.
Maisha ya kuishi pekee hakuyaweza, aliamua kusafiri hadi Bukoba kwa Beatrice ili ampeleke kwa wazazi wake kujitambulisha. Alifika Bukoba siku ya Jumamosi na jioni ya siku iliyofuata Beatrice alimpeleka Mike kijijini kwao Kanyigo kuonana na wazazi wake.
***
"Msigazi murungi nabasa kumshwela muhala waitu Beatrice." (Ni kijana mzuri anafaa kuwa mume wa binti yetu Beatrice) mama yake Beatrice alisema.
"Nanye nimbona asaine chonka munyamahanga, Msukuma.” (Na mimi naona anafaa lakini si mtu wa kabila letu, ni Msukuma).
Mzee Rugakingira, baba mzazi wa Beatrice aliitikia.
"Okuba Msukuma ti nshonga boona bashaija." (Kuwa Msukuma si tatizo, wote ni wanaume tu kama wengine), mama alimalizia.
Mzee Rugakingira na mkewe walikaa pembeni kumjadili Mike baada ya kutambulishwa kwao na Beatrice.
Baada ya chakula cha usiku wazazi wa Beatrice walimkubali Mike na kutoa baraka zao zote, ilikuwa furaha kubwa kwa Beatrice.
Mike hakuamini kama ingekuwa rahisi kiasi hicho kwani alishaambiwa kuwa watu wa mkoa wa Kagera walipendelea sana kuoana wao kwa wao, yaani watu wa kabila moja! Hakutegemea kama wangeweza kumkubali yeye Msukuma mara moja.
Pamoja na kukubali kwao kirahisi, wazazi wa Beatrice waliwasisitizia umuhimu wa kupimwa UKIMWI, kabla ya ndoa. Walidai kuwa wakati huo UKIMWI ulikuwa tishio kubwa sana kwa mkoa wa Kagera na Tanzania nzima.
Si Beatrice wala Mike aliyetiwa hofu na suala hilo la kupima UKIMWI, hiyo ilitokana na ukweli kwamba hadi umri waliokuwa nao hakuwepo mmoja kati yao aliyewahi kukutana kimwili na mtu mwingine.
Walikuwa wakisubiri siku ya ndoa yao kwa hamu ili wapate kukionja kitendo hicho.
Kabla ya kuondoka Bukoba, Mike alifanya mipango yote ya kumhamishia Beatrice mjini Mwanza kikazi ili apate kuwa karibu naye wakati wakikamilisha mipango yao ya ndoa.
Baada ya ya kufika Mwanza, Mike aliwataarifu wazazi wake ambao kwa muda mrefu aliwaficha mipango yake ya kumwoa Beatrice. Wazazi wake walifurahi sana na moja kwa moja wakatoa baraka zao zote. Mzee Martin akaahidi kusafiri yeye na wazee wengine maarufu mjini Mwanza kwenda Bukoba kufahamiana na wazazi wa upande wa pili na pia kutoa mahari.
***
Taarifa za harusi ya Mike zilipoanza kutapakaa mjini Mwanza watu wengi hawakuamini. Kwa muda mrefu watu wengi waliamini Mike alikuwa na kasoro ya kimaumbile, kwani tabia ya Mike kutojihusisha na wanawake ndiyo iliyosababisha watu kuamini hivyo.
Mzee Martin aliporudi kutoka Bukoba vikao vya harusi vilianza na kadi za michango zilisambazwa kwa kila mtu aliyekuwa karibu na Mike na familia yake. Watu wakawa na hamu kubwa ya kuishuhudia ndoa ya Mike na Beatrice.
Huko Bukoba pia taarifa zilisambaa kila kona na kwa ndugu wote na marafiki wa familia ya Rugakingira.
Hata wafanyakazi wenzake katika hospitali ya Mkoa wa Kagera walitaarifiwa. Michango ilianza kutolewa. Kwa jinsi pesa zilivyochangishwa, watu walishindwa kuelewa ukubwa wa harusi hiyo ungekuwa vipi.
***
Miezi miwili baadaye Beatrice alihamia mjini Mwanza. Alifikia Capri Point, kwa dada yake mkubwa, Margareth, mke wa Samson, mfanyabiashara maarufu mjini Mwanza. Baada ya kufika Mwanza, Mike alimtafutia kazi hospitali ya Bugando ambako alifanya kazi kama Muuguzi Mkunga kama ilivyokuwa Bukoba.
Kwa sababu ya ukaribu, mawasiliano kati yao yakawa makubwa. Walionana karibu kila siku, ambapo Mike alipotoka kazini alikuwa na kawaida ya kupitia hospitali kumchukua Beatrice na kumrudisha nyumbani kwa dada yake.
Kila mtu aliyewaona Mike na Beatrice alikiri kweli walipendana na walikuwa mfano wa kuigwa. Siku za mwishoni mwa wiki kila walikokwenda walikuwa wawili, tena mkono kwa mkono! Kila mtu mjini Mwanza alitamani kuiona ndoa yao.
***
Wakati homa ya harusi ya Beatrice na Mike ikiwa imepanda kupitia kiasi mjini Mwanza, mzee Rugakingira alipiga simu kutoka Bukoba na kuwakumbusha Mike na Beatrice juu ya kupima UKIMWI.
Ili kuonyesha kuwa hawakulidharau ombi la wazazi, siku iliyofuata asubuhi na mapema wote wawili wakaenda hospitali ya Bugando kushughulikia suala hilo.
"Sijui baba hatuamini!" Beatrice alihoji kwa utani wakiwa njiani kuelekea Bugando.
"Si unajua tena wazee wetu, si ajabu wananitilia mashaka mimi au naonekana mhuni sana nini?" Mike alitania.
Walinyoosha moja kwa moja hadi hospitali ya Bugando, baada ya kuegesha gari walipitiliza moja kwa moja hadi maabara ambako waliandikisha majina yoa na kupanga foleni, wakisubiri kuitwa.
Muda mfupi baadaye mwanamke mmoja mfupi alichungulia kutoka mlango wa maabara.
"Mike Martin na Beatrice Rugakingira, tafadhali ingieni!" Ilikuwa ni sauti ya muuguzi akiwataka waingie maabara.
Wote wawili walinyanyuka na kuingia maabara ambako walichukuliwa vipimo. Baada ya shughuli hiyo, Mike alimrudisha Beatrice nyumbani, kwa dada yake.
Siku hiyo Beatrice alitaka kuingia zamu ya mchana, hivyo alipomfikisha kwao aliondoka kwenda kazini kwake eneo la viwanda vya Nyakato, barabara ya kuelekea Musoma.
Maisha yaliendelea kama kawaida huku watu wakiendelea kuchanga maelfu ya shilingi kwa ajili ya harusi hiyo ya aina yake. Harusi iliyotegemewa kufungiwa angani ndani ya ndege ya Shirika la Ndege la Precision wakati maelfu ya watu wakishuhudia na kushangilia kwa chini.
***
"Siamini!" Mike alisema huku machozi yakimtoka.
"Nimeutoa wapi mimi?" Aliendelea kujiuliza maswali bila kupata majibu.
"Huu ni uongo mkubwa," alisema kwa sauti ya juu mpaka baadhi ya watu waliokuwa karibu naye wakasikia, palepale alinyanyuka na kumkaba shati daktari aliyekuwa akimpa unasihi.
"Kwa nini mnanipakazia, hamtaki nimuoe Beatrice siyo?"
"Mike wewe ni kijana unayeheshimika sana hapa mjini, tafadhali usifanye jambo hilo." Mmoja wa wauguzi waliokuwa maabara alisihi katika kujaribu kuituliza hali hiyo kabla watu hawajakusanyika kusikiliza.
"Haiwezekani, kwa nini mnisingizie kitu kama hiki mimi wakati sijawahi kukutana na mwanamke yeyote maishani mwangu? Iweje leo mniambie habari kama hii?"
"Sio hivyo kaka, tuliza moyo kwanza!" Muuguzi aliyekuwa pale aliendelea kusihi.
Mike alivikunjua tena vile vyeti vya majibu na kuanza kuvisoma kwa mara ya pili. Alikuwa haamini kabisa kama majibu yake yalionyesha alikuwa “Elisa Test Positive,” yaani alikuwa na virusi vya UKIMWI na majibu ya Beatrice yalionyesha “Elisa Test Negative,” yakiwa na maana hakuwa na virusi vinavyoambukiza UKIMWI.
"Nimeutoa wapi mimi?" Mike aliendelea kuuliza kwa sauti.
Kwa kasi ya ajabu Mike alitoka maabara na kukimbia hadi nje ya geti, akaingia ndani ya gari lake na kuliondoa kwa mwendo wa kasi kuelekea eneo la Isamilo. Alinyoosha moja kwa moja hadi kwenye majengo ya kitengo cha uchunguzi cha kitabibu cha Medical Research.
Aliyemfuata huko hakuwa mwingine bali ni Dkt. Mazira, mmoja wa marafiki zake wa karibu waliyesoma wote Shule ya Sekondari ya Nsumba.
"Ee bwana mbona macho mekundu, umefiwa?" Dkt. Mazira aliuliza mara tu baada ya kumwona Mike.
Mike alianza kulia tena.
"Bwana, mimi nimetoka Bugando, hapa nilipo nimechanganyikiwa kiasi cha kutosha."
"Kuna nini cha kukuchanganya Mike?"
"Majibu!"
"Majibu ya nini?"
"Ya UKIMWI, eti yameonyesha mimi Positive na Beatrice ni Negative hizi si njama za kukwamisha ndoa yetu, kweli? Siamini hata kidogo, nimekuja kwako ili turudie kupima?”
"Hebu njoo huku ndani."
Waliingia ndani ambako kwa haraka Dkt. Mazira alimtoa Mike damu na kuanza kuifanyia uchunguzi.
"Nisubiri hapo hapo!" Dkt. Mazira alisema.
Dakika arobaini baadaye Mike alishangazwa na jinsi macho ya Dkt. Mazira yalivyokuwa yametoka, alionyesha wasiwasi mkubwa.
"Nini daktari?"
"Hapana Mike ni kitu cha kawaida tu."
"Please tell me, is it positive or negative? That's what I want to know!" (Niambie, daktari, nina virusi au sina, hicho ndicho ninachotaka kujua).
"Ah! Ah! Ah!..." daktari alishikwa na kigugumizi.
"Niniiii?"
"Kwa kweli, Mike ni suala gumu kidogo kukueleza, nafikiri tunahitaji kurudia tena baada ya wiki tatu, kuna wakati hivi vipimo vyetu huwa vinatoa majibu yasiyo kweli?”
“Hivyo ina maana kwa leo imeonyesha mimi ni positive?” Mike aliuliza.
"Hivyo ndivyo rafiki yangu, siwezi kukuficha kitu lakini ninategemea utasimama imara katika kipindi chote tukisubiri kurudia vipimo!"
Mike aliinama na kuanza kulia tena, Dkt. Mazira alijaribu kumbembeleza lakini haikuwezekana Mike akaondoka bila kuaga na kuingia ndani ya gari lake na safari ya kuelekea nyumbani kwake ikawa imeanza.
Mike hakumwambia Beatrice habari za majibu hayo ingawa Beatrice aliingiwa na hofu kwa jinsi alivyoona mabadiliklo ya tabia ya mpenzi wake. Mike alikuwa ni mwenye huzuni kubwa na mara nyingi alikuwa akitokwa na machozi.
"Mike una tatizo gani?” Kila siku Beatrice aliuliza.
"Mimi? Sina matatizo yoyote, nina mafua tu!" Mike alitumia jibu hilo kila alipoulizwa kuhusu afya yake.
Wiki tatu baadaye Mike alikuwa tena Medical Reseach ambako Dkt. Mazira alichukua tena damu yake kwa ajili ya kupima. Majibu yalipotoka yalionyesha Mike alikuwa Positive vilevile!
Mike alilia machozi kwa uchungu na alishindwa kuelewa jibu la Positive lilitoka wapi, wakati maishani mwake hakuwahi kufanya ufuska wowote wala kutembea na mwanamke yeyote! Kitu kingine kilichomchanganya zaidi akili ni lugha gani angeitumia kuwafahamisha watu ambao tayari walishachanga pesa zao kwa ajili ya harusi yake. Je, angewaambia hataoa tena kwa sababu ana virusi vya UKIMWI? Alishindwa kupata jibu la moja kwa moja angetumia njia ngani kumwelewesha Beatrice kuwa ndoa isingewezekana tena kwa kuwa yeye alikuwa anaishi na virusi.
Kila alipoufikiria muda ambao Beatrice aliupoteza kumsubiri, alijihisi vibaya, aliulaani UKIMWI na kwa nini ulikuja duniani. Alikumbuka kuwa Beatrice alikwishakataa wachumba watatu wakati Mike akiwa Uingereza. Alishindwa kuelewa Beatrice angejisikia vipi wakati tayari alikwishawaeleza marafiki zake wote kuhusu ndoa yake na wengine tayari walishaanza kushona sare za harusi.
Mike alibaki ameduwaa bila kujua la kufanya, hakuwa tayari kuua kiumbe kisicho na hatia. Hakutaka kumuua Beatrice kwa sababu alimpenda mno! Alimshukuru Mungu kwa sababu yeye na Beatrice walikuwa hawajawahi kujamiiana tangu wafahamiane, vinginevyo hata Beatrice angekuwa Positive.
Alipofikiria ni wapi alikoupata ugonjwa huo bado hakupata jibu. Jibu lililomjia kichwani kwa haraka ni hisia juu ya damu ya Laila! Damu ile aliitilia shaka sana.
"Nitakwenda hadi Mogadishu nikamtafute Laila ili nihakikishe kama ni kweli yeye ndiye aliyeniambukiza,” alijisemea Mike. Alikumbuka kuwa Laila aliwahi kumweleza kuwa baba yake mzee Mohamed alikuwa mtu maarufu sana mjini Mogadishu.
"Hivyo ni rahisi sana kumpata na nikikuta ni kweli sijui nitampa adhabu gani...! Hakuna sababu ya kumwadhibu Laila nia yake ilikuwa njema alitaka kuokoa maisha yangu.”
Wakati Mike akiwaza yote hayo, tayari alikwishaondoka Medical Research. Gari lake aliligesha kando ya barabara ya kwenda uwanja wa ndege. Kutokana na kuelemewa na mawazo alijikuta usingizi umempitia humohumo ndani ya gari. Aligutuka saa kumi jioni baada ya kupigiwa honi na gari la wafanyakazi wa kiwandani kwake, walishangaa kumkuta bosi wao mahali pale.
Alikuwa amelala ndani ya gari hilo kwa saa tano! Alipokumbuka kilichomfanya awe pale na katika hali ile, alianza kulia tena. Baadaye kwa taabu aliliondoa gari lake kwa kasi ya ajabu kuelekea nyumbani kwake, Bugando.
Mike alianza kuamini ukweli kuwa UKIMWI ulikuwa na tabia ya kuwaua vijana mara tu wanapopata mafanikio katika maisha yao!
Alipata mafanikio makubwa katika maisha yake na sasa alitakiwa kufa na kuviacha vyote alivyokuwa navyo. Mbele yake aliona giza nene, tena aliziona siku zake za kuiaga dunia hazikuwa mbali naye, machozi yakamtoka.
Aliamini hapakuwa na mtu aliyeuogopa UKIMWI duniani kama yeye lakini sasa alikuwa nao na hakujua angewaeleza nini watu ili waamini kuwa katika maisha yake hakuwahi kutembea na mwanamke.
Aliamini kila mtu angemwona malaya kwa sababu ndivyo jamii ilivyouchukulia ugonjwa huo. Mike alitamani kujiua kwa kuogopa aibu hiyo. Alipofika nyumbani kwake aliingia ndani na moja kwa moja alikwenda mezani ambako alichukua kalamu na karatasi na kuanza kumwandikia barua Beatrice.
Mpenzi Beatrice,
Naandika barua hii nikiwa katika majonzi makubwa na machozi yakinitoka, Beatrice, jambo ninalotaka kukueleza si rahisi wewe kuliamini hata kidogo lakini ndivyo ilivyo. Najua litakuumiza zaidi lakini inabidi niseme ili angalau nipate faraja kutoka kwako! Nitakuficha hadi lini wakati hiki ni kifo?
Naikumbuka siku ya kwanza tulivyokutana shuleni Nsumba miaka mingi iliyopita, tangu siku hiyo hadi leo ni kama miaka kumi au zaidi.
Tangu wakati huo umenisubiri ili tuoane, tuzae watoto na kujenga familia yetu. Hilo limekuwa kweli, na wazazi wetu wametupa baraka zao na lilikuwa tegemeo letu kuwa siku chache zijazo tungefunga ndoa.
Beatrice, inaniuma kukueleza kuwa HATUTAOANA TENA!! Si kwamba nakuchukia, la, ila sitaki kuua kiumbe kisicho na hatia!
Beatrice, uamuzi huu unatokana na yale majibu ya damu tulivyokwenda kupimwa. Hayo ndiyo yaliyosababisha yote haya. Amini, usiamini, Beatrice, sijawahi kukutana na mwanamke kimapenzi katika maisha yangu na ndiyo maana siku zote huwa nasema ninaweza kuitwa “bikira wa kiume.”
Lakini cha ajabu na cha kushangaza majibu yameonyesha mimi nina virusi vya UKIMWI wewe huna! Nilipoyaona majibu haya sikuamini, ikabidi niende Medical Research kurudia vipimo, lakini nako majibu yakawa ni hayohayo. Leo tumepima kwa mara ya tatu bado mimi nimeonekana nina virusi, hivyo nimelazimika kuuchukua huo kama ukweli wenyewe.
Beatrice, ninakupenda na namshukuru Mungu katika maisha yetu ya kufahamiana hatukuwahi kuingia majaribuni na kufanya mapenzi. Je, unaikumbuka siku ile pale bafuni Natta Hotel? Kama tungemruhusu shetani na kufanya tendo la ndoa, wewe pia ungekuwa positive.
Sasa basi, kwa vile bado hujaambukizwa mimi sioni sababu ya kukuua Beatrice! Ni heri tuachane ili uolewe na mtu mwingine yeyote na uwe na familia yako. Naomba uniache mimi nife peke yangu. Nafikiri hivyo ndivyo Mungu alivyopanga.
Samahani Beatrice kwa kukupotezea muda wako mwingi lakini nitakulipa fidia kidogo. Nitakupa shilingi milioni kumi na gari moja lenye tela, hizo zitakuwa mali zako mwenyewe na zitakusaidia maishani.
Sina mengi ya kusema bali nakutakia maisha marefu popote. Wewe ni msichana mzuri, nina imani utapata mtu mwingine wa kukuoa na uzae watoto wazuri. Naomba ukizaa mtoto wa kiume umwite Mike kwa kumbukumbu yangu.
Asante.
Ni mimi katika majonzi,
Mike.
Je nini kitaendelea?
RNGM blog

No comments